1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matokeo ya michezo mwishoni mwa Juma

Mohammed AbdulRahman15 Oktoba 2007

Ujerumani yajikatia tiketi ya fainali za kombe la kandanda la mataifa ya Ulaya mwakani, Bingwa wa zamani wa uzani wa juu duniani Evander Holyfield ashindwa katika jaribio lake la kurudi tena kileleni na Uganda yashindwa kufuzu kwa fainali za kombe la kandanda la Afrika huko Ghana

https://p.dw.com/p/C7nN
Kombe la mataifa ya Ulaya litakaloaniwa mwakani 2008
Kombe la mataifa ya Ulaya litakaloaniwa mwakani 2008Picha: pa / dpa

Wakati michuano ya ligi kuu ya Ujerumani Bundesliga ilisimama mwishoni mwa juma kwa sababu ya michuano ya kusaka tiketi ya kucheza fainali za kombe la mataifa ya ulaya mwaka ujao, huku Bayern Munich ikiongoza ligi hiyo,Ujerumani tayari imeshajinyakulia tiketi ya kucheza fainali hizo -mashindano yatakayofanyika kwa ubia huko Austria na Uswisi. Ujerumani ilitoka sare na Ireland mjini Durblin bila kufungana na matokeo hayo yalitosha kuiweka ileleni katika kundi D, ikiwa na jumla ya pointi 23 baada ya mechi 9,wakati Ireland iliocheza mechi 10 ina pointi 14 ikishika nafasi ya tatu. Ujerumani itamenyana na Jamhuri ya Cheki .Jumatano katika mechi ambayo itakua sehemu yakumalizia ratiba tu.Jamhuri ya Cheki inashika nafasi
ya pili katika kundi hilo ikiwa imecheza pia mechi
9 na ina pointi 20. Timu mbili za kwanza katika
kila kundi ndizo zitakazocheza hatimae katika
fainali hizo.

Akizungumzia mechi hiyo dhidi ya Ireland, Kocha wa Ujerumani Joachim Loew alisema,

“Tulishinda mechi ya kwanza na Ireland nafikiri Septemba mbili. Leo tayari tumefanikiwa zikiwa zimebakia mechi tatu kabla ya kinyanganyiro hiki kumalizika”

Naye mshambuliaji Kevin Kurani alikua na haya ya kusema akielezea matumaini akaongeza kuwa,“ Natumai kama tutacheza kama tulivyofanya mechi zilizopita, tunaweza kufika hadi fainali.”

Kinyanganyiro lakini kiko katika kundi la pili-kundi
B ambamo kuna mabingwa wa dunia Italia na makamu Ufaransa. Inayoongoza kundi hilo ni Scotland ikiwa na point 24 ikifuatiwa na Italia pointi 23 na Ufaransa pointi 22 .Zote zimechacheza mechi 10. Jumamosi Scotland iliizamisha Ukraine mabao 3-1, na Italia i nayo ikicheza pia nyumbani kicharaza Georgia mabao 2-0.

Ufaransa ikamaliza kiu chake cha magoli kwa kuvitandika visiwa vya Faroe nyumbani kwao mabao 6 kwa yai.katika kundi hilo Scotland,
Italia na Ufaransa kila moja najiwekea matumaini ya kuweza kukata tiketi ya fainali za kombe la mataifa ya ulaya.

Msisimko mwengine ni katika kundi la tatu kundi C,kati ya Ugiriki inayoongoza kundi hilo, Uturuki
nafasi ya pili na Norway ya tatu ikitanguliwa na Uturuki kwa pointi 1 tu. Wakati Uturuki iliitandika Bosnia Herzogovina 3-2 , Uturuki
ilikua na kai mbele ya Moldavia na hatima kuambulia sare ya 1-1. Uturuki watawakaribisha majirani zao.Ugiriki katika mechi inayosubiriwa kwa hamu Jumatano ijayo.

Uingereza imejiongezea matumaini ya kusonga mbele na kufanikiwa kucheza fainali, baada ya kurudi mshambulцiaji hatari Wayne Rooney aliyekua kwenye orodha ya majeruhi. Rooney alipachika bao la pili katika ushindi wa England wa mabao 3-0 dhidi ya Estonia, wakati Croatia inayoongoza kunde hilo mbele ya England iliifunga Israel 1-0 . England itamenyana na Russia inayoshika nafasi ya tatu katika mechi ijayo ya kundi hilo la E hapo Jumatano.

Kundi F ni Sweden inayoshika usukani na
kujiimarisha zaidi kwa ushindi wa mabao 3-0 mbele ya Lithuania, ikifuatiwa na Uhispania ,iliotamba pia
ugenini kwa kuibwaga Denmark mabao 3-1 ,matokeo yaliomaanisha kwamba Denmark ilioshiriki mara sita mfululizo katika fainali ya kombe la mataifa ya Ulaya ,imetolewa katika fainali zijazo.

Rumania ndiyo inayoshika uongozi katika kundi G baada ya kuilaza Uholanzi inayoifuata kwa tafauti ya pointi tatu, bao moja kwa bila mjini Bucharest.
Rumania ina jumla ya pointi 23.
Luxembourg inayokamata mkia katika kundi hilo,
hatimae ilikua na sababu ya kusherehekea ilipoondoa ukame wa kutoshinda hata mechi moja kati ya 9 zilizotangulia na kuilaza kwao Belaruss bao 1-0 na kujinyakulia pointi 3 za kwanza.

Rugby:

Fainali za kombe la duniani la mchezo wa Rugby
itakua ni kati ya England na Afrika kusini .Katika mchuano wa kukata na shoka Jumamosi mjini Paris mbele ya umati mkubwa wa watazamaji, England iliwalaza wenyeji Ufaransa 14 kwa 9.Ufaransa ilikua ikiongoza 9-8 hadi dakika 6 kabla ya mchezo kumalizika,lakini kwa mshangao wa mashabiki wake,mambo yakabadilika katika muda huo na England hatima
kuibuka na ushindi. Katika nusu fainali nyengine,
Timu ya taifa ya Rugby ya Afrika kusini maarufu kwa jina la Springboks ikaibwaga Argentina 37-13 na sasa suali linaloulizwa ni jee England itaweza mwishoni mwa juma hili kulitetea taji lake na kurudi na kombe hilo mjini London, au Afrika kusini itavuka nalo kutoka anga ya Ulaya kuelekea mjini Johannesburg ?




Barani Afrika,timu ya taifa ya Uganda The Cranes nayo imejiunga na
Taifa Stars ya Tanzania na Harambee Stars ya Kenya na kushindwa kufanikiwa kucheza fainali za kombe la mataifa ya Afrika-mashindano yatakayofanyika mwakani nchini Ghana. Uganda ikitegemea timu moja wapo kati ya Benin na Mali ipoteze mechi ya Jumamosi iweze kufanikiwa ,
lakini matumaini hayo kwa Waganda walioshinda mechi zote za nyumbani, kwenda sare mbili ugenini na kufungwa mechi moja, yalikatika baada ya Benin kuifunga Sierra leone mjini Free town mabao 2-0 na Mali nayo pia kushinda ugenmini dhidi ya Togo mabao 2-0. Uganda hata hivyo ilikua karibu zaidi safari hii katika kiu chake cha miaka karibu 30 kuwania kucheza
fainali za kombe la Afrika, na sasa inabidi isubiri
kujaribu tena miaka miwili ijayo.

Ubondia:
Bingwa wa zamani wa masumbwi uzito wa juu,
Mmarekani Evander Holyfield, ameshindwa katika jaribio lake la kunyanganya taji la ubingwa wa dunia shirika la ndondi la WBO Sultan Ibragimov wa Urusi. Siku 6 kabla ya kusherehekea siku yake ya kuzaliwa na kutimiza miaka 45, Holyfield akishindwa nma Mrusi
huyo mwenye umri wa miaka 35 kwa pointi katika
pambano lao la Jumamosi la raundi 12 mjini Mosko. Waamuzi wote watatu walimpa ushindi Ibragimov, aliyekua akilitetea taji hilo kwa mara ya kwanza tangu alipolinyakua mwezi Juni mwaka huu.