1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mataifa yenye kura ya turufu yanavyozuwia mataifa mengine kujiunga na umoja wa mataifa.

Sekione Kitojo14 Julai 2007

Matumizi ya kura ya Veto, turufu, kuzuwia baadhi ya nchi kupata uanachama wa umoja wa mataifa, masalio ya vita baridi, yanatishia kurejea tena katika siasa za taasisi hiyo muhimu ya dunia.

https://p.dw.com/p/CHAw

Marekani inatarajiwa kuwasilisha azimio katika baraza la usalama la umoja wa mataifa , huenda wiki ijayo ama kabla ya mwisho wa mwezi huu, linalotaka Kosovo kuwa mwanachama wa umoja wa mataifa, jimbo la zamani la Yugoslavia ya zamani.

Lakini Russia , taifa linalotokana na Urusi ya zamani inatishia kutumia kura yake ya turufu kuzuwia jimbo hilo linalotawaliwa na umoja wa mataifa la Kosovo kuwa mwanachama wa chombo hicho cha dunia.

Marekani inasisitiza kuwa baraza la usalama la umoja wa mataifa lenye wanachama 15 linapaswa kuchukua hatua juu ya Kosovo haraka iwezekanavyo, lakini Russia , mshirika wa karibu wa Serbia , inataka kuzuiwa kwa pendekezo hilo. Russia inapinga hatua ya jimbo hilo la Kosovo linalokaliwa na wakaazi wengi wenye asili ya Albania kujitenga kutoka Serbia . lakini muafaka wa kisiasa kwa hivi sasa unafanyika katika mazungumzo ya faragha .

Mkwamo kama huo unaweza kujitokeza iwapo na wakati kutakuwa kuvunjika kwa Iraq katika majimbo matatu, ya Washia, Sunni na Wakurdi, wakati kuna mataifa mengine yanayoweza kuzuka , ikiwa ni pamoja na Sahara ya magharibi na jimbo linalotaka kujitenga nchini Moldovan la Trans-Dniester pamoja na jimbo nchini Georgia la South Ossetia, kwa mujibu wa wanadiplomasia wa umoja wa mataifa.

Mataifa haya yote yanaweza haraka ama baadaye kuzusha mvutano wa kisiasa baina ya Russia na Marekani katika taasisi hiyo ya kimataifa, hususan katika umoja wa mataifa kuzitambua nchi hizo.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Russia Sergei Lavrov ametupilia mbali juhudi za Marekani za kutatua mzozo wa Kosovo kwa kuuliza swali, kwa nini hatutatui suala la Sahara magharibi kwanza ? Mzozo ambao umekuwapo kwa muda wa miaka mingi ambapo Marekani inaunga mkono mshirika wake Morocco dhidi ya chama cha Polisario kinachodai uhuru wa jimbo hilo kaskazini ya Afrika.

Kileleni mwa vita baridi katika miaka ya 1960 na 70 mataifa hayo yenye nguvu yalipunga kura zao za turufu kwa kiburi na mara kwa mara bila sababu ya maana , na kuyazuwia mataifa kuwa wanachama wa umoja wa mataifa hususan kutokana na sababu za kisiasa ama kulinda maslahi yao ya kitaifa.

Marekani iliyazuwia mataifa ambayo yanaonekana kuwa washirika wa Urusi na Russia imezuwia mataifa yanayoonekana kuwa ama marafiki wa Marekani ama maswahiba wa kisiasa wa mataifa mengine ya Ulaya kama Uingereza na Ufaransa, wanachama wengine wawili wenye kura ya turufu katika baraza la usalama la umoja wa mataifa.

Iwapo taifa lolote huru lina haki ya kuwa mwanachama ama la hii haina umuhimu.

Warusi walitumia mantiki ya siasa za vita baridi kuizuwia Itali kuwa mwanachama wa umoja wa mataifa kwa kupiga kura ya veto kwa karibu mara sita na pia dhidi ya Japan mara nne.

Marekani nayo , kwa upande wake ilitumia kura ya turufu mara saba ikiizuwia Vietnam kuingia katika taasisi hiyo ya kimataifa , na ikapiga kura mara moja dhidi ya Angola baada ya kupata uhuru, nchi zote hizo zina mahusiano ama ya kijeshi ama ya kisiasa na Urusi.

Akulizwa iwapo kitisho cha kutumia kura ya turufu dhidi ya Kosovo ni marejeo ya siku za vita baridi, Stephen Zunes , profesa wa siasa katika chuo kikuu cha San Francisco Marekani amesema , hii inaonekana kuwa hizo ni nadharia za kushuku.