1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi makali yaendelea Hodeidah

8 Novemba 2018

Mamia ya wapiganaji wameuliwa huku majeshi ya serikali yakiyakabili majeshi ya waasi katika nji wa Hodeidah nchini Yemen. Madaktari katika hospitali za eneo hilo wamesema waasi 47 waliuliwa kufuatia mashambulio ya angani

https://p.dw.com/p/37tcN
Yemen - Schulweg in Taiz
Picha: DW/K. Al Banna

Shirika la Kimataifa la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limewalaumu waasi wa Yemen kwa kuzifanya hospitali kuwa kambi za kijeshi, huku ikizitaka pande zinazotofautiana kuwalinda raia. Amnesty imesema waasi wa Huthi waliwapeleka wapiganaji kwenye paa la hospitali moja eneo hilo mnamo tarehe 22 mwezi Mei mwaka huu wa 2018, hatua waliyoitaja kukwamisha maendeleo.

Mkuu wa kampeni za shirika la Amnesty eneo la Mashariki ya Kati, Samah Hadid, amesema hatua ya waasi kuwapeleka wanajeshi wao katika paa la hospitali inakiuka sheria za kimataifa. Waasi wamekuwa wakiudhibiti mji wa Hodeidah tangu mwaka 2014 wakati walipouteka mji mkuu Sanaa.

Hayo yakijiri, Mkuu wa waasi Abudlmalik al- Huthi ameapa kutojisalimisha kwa majeshi yanayoungwa mkono na Saudi Arabia. Kwenye hotuba yake iliyopeperushwa kupitia televisheni al-Huthi amekiri kuwa amezidiwa nguvu lakini akaashiria kutobabaishwa na hatua hiyo. Aidha aliwataka raia wa Yemen kuunga mkono kampeni za Wahuthi nchini humo. "Nawaomba kila raia kushirikiana na kuwaeleza kuwa leo tuna jukumu la kukabili uchokozi unaoelekezwa katika mipaka na maeneo mengine. Kila mtu ana wajibu wa kuunga mkono ajenda ya kijeshi kwa sababu ina umuhimu, yenye maamuzi na ya msingi. Hakuna hatari isipokuwa kwa wasiojali na wadhaifu."

Marekani ambayo inatoa usaidizi wa vifaa kwa majeshi ya muungano wa Saudi, wiki iliyopita walishauri mapigano hayo yasitishwe lakini hilo halijatimia. Msemaji wa serikali Robert Palladino amesema Marekani imerejelea kauli yake kwa pande husika kuwa hakuna ushindi wa kijeshi utakaopatikana nchini Yemen.

Takriban raia elfu kumi wa Yemen wameuawa tangu mwaka 2015, kulingana na Shirika la Afya Duniani WHO. Hayo yanajiri wakati nchi hiyo ikikabiliwa na hatari ya kushuhudia ukame.

Mwandishi: Sophia Chinyezi/AFPE
Mhariri: Mohammed Khelef