1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yachukizwa na ushuru wa China

Lilian Mtono
3 Aprili 2018

Marekani imeutaja ushuru wa forodha uliowekwa na China kwenye bidhaa zake kama "sio haki", baada ya China kuweka ushuru wa bidhaa 128 zenye thamani ya dola bilioni 3, zinazoingizwa na Marekani nchini humo.

https://p.dw.com/p/2vQk3
USA Trump besiegelt Strafzölle auf Stahl und Aluminium
Picha: Getty Images/AFP/M. Ngan

Marekani imeutaja ushuru wa forodha uliowekwa na China kwenye bidhaa zake kama "sio haki", baada ya China kuweka ushuru wa bidhaa 128 zenye thamani ya dola bilioni 3, zinazoingizwa na Marekani nchini humo, zinazojumuisha matunda na nyama ya nguruwe, ikiwa ni hatua za karibuni zaidi za ulipizaji kisasi kufuatia Marekani kupandisha ushuru wa bidhaa za chuma cha pua na bati. 

Hatua hiyo ya China, iliyofikiwa na tume ya taifa ya ushuru wa forodha ya China, imekuja baada ya wiki kadhaa ya vita vya maneno iliyoibua wasiwasi wa vita vya kibiashara kati ya mataifa hayo yenye nguvu zaidi kiuchumi duniani. 

Serikali ya rais Donald Trump imesema ushuru wake ulilenga bidhaa za chuma cha pua na bati zinazoingizwa nchini Marekani ambazo ilizichukulia kama kitisho dhidi ya usalama wa taifa hilo, lakini wizara ya biashara ya China imeiita sababu hiyo kuwa ni kile ilichosema "ukiukwaji" wa miongozo ya shirika la kimataifa la biashara, WTO.

Trump mara kadhaa aliishambulia China akidai hupata ziada kubwa itokanayo na biashara kati yake na Marekani na aliahidi katika kipindi cha kampeni kuchukua hatua za kupunguza hali hiyo. 

China Fabrik in Anhui - Aluminium
Bidhaa za bati zinazozalishwa China ni miongoni mwa bidhaa zilizoongezewa ushuru na MarekaniPicha: picture-alliance/AP Photo/Chinatopix

Naibu msemaji wa ikulu ya White House Lindsay Walters alinukuliwa akisema kwamba utoaji wa ruzuku wa China na muendelezo wa kuzalisha bidhaa kwa wingi ndio mzizi wa mzozo uliopo. Aliongeza kuwa badala ya China kulenga bidhaa za Marekani zinazouzwa nje kihalali, inatakiwa kuacha mpango wake usio wa haki wa kibiashara, ambao unaathiri usalama wa ndani wa Marekani na kuharibu masoko ya kimataifa.

Taarifa ya wizara ya mambo ya biashara ya China, ilisema wanataraji kwamba Marekani itaondoa hatua zinazokiuka kanuni za WTO haraka iwezekanavyo ili kurejesha mazingira bora ya kibiashara kwa bidhaa zinazotoka na kuingizwa kati ya Marekani na China. 

Hii leo, waziri wa mambo ya kigeni wa Japan Taro Kano akiwa mjini Tokyo ameelezea wasiwasi wake kwa waandishi wa habari kuhusiana na hatua hizo za kisasi kati ya Marekani na China, na kusema kwamba zinaweza kuwa na matokeo makubwa kiuchumi.

Waziri Kano amesema kwamba nafasi ya Japan katika mzozo huo ni kuhakikisha inalinda mfumo wa biashara huru ambayo ilianzishwa na shirika la biashara duniani, WTO. Ameongeza kuwa waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe atamkumbusha rais Donald Trump kuhusu nafasi yake wakati wa ziara yake nchini Marekani katikati ya mwezi huu wa Aprili. 

Marekani, ilisimamisha kwa muda ushuru wa forodha kwa bidhaa zinazotoka mataifa ya Umoja wa Ulaya, pamoja na Argentina, Brazil, Canada, Mexico na Korea Kusini. Lakini ikulu ya White House iliweka wazi mipango yake ya kuziwekea ushuru mpya bidhaa zinazoingizwa kutoka China, za kiasi cha dola bilioni 60, dhidi ya kile ilichokitaja kama "wizi" wa haki miliki.   

Makamu waziri mkuu wa China Liu He, ambaye ni afisa wa juu wa masuala ya uchumi alimueleza waziri wa fedha wa Marekani Steven Mnuchin katika mazungumzo kwa njia ya simu kwamba uchunguzi wa kibiashara ulikiuka kanuni za biashara za kimataifa na China ilikuwa tayari kulinda maslahi ya taifa hilo.  

Mwandishi: Lilian Mtono/DPAE/AFPE/APE
Mhariri: Josephat Charo