1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hakuna kurudi nyuma Burundi

18 Mei 2015

Hakuna njia nyingine ila kusonga mbele nchini Burundi katika harakati za kuitekeleza katiba ya nchi.Hayo anasema mwandishi wetu Claus Stäcker katika maoni yake.

https://p.dw.com/p/1FQQn

Rais Pierre Nkurunziza ambae hapo awali alikuwa kiongozi wa waasi kwa mara nyingine amethibitisha kwamba yeye ni kamanda hodari wa kijeshi.Amefanikiwa kuwazuia wanajeshi waasi kumwondoa madarakani. Na jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki imeshikamana naye katika kipindi chake kigumu.

Waziiri wa mambo ya nje wa Tanzania Bernard Membe amesema bara la Afrika halitaki kumwona kiongozi anaetwaa mamlaka ya nchi kwa kutumia nguvu za kijeshi. Umoja wa Afrika pia ulililaani jaribio la kumwondoa Nkurunziza madarakani. Umoja wa Afrika umelishutumu jaribio la wanajeshi la kutaka kutwaa mamlaka kwa njia ya mabavu.

Kauli hizo zingekuwa za kutia moyo laiti bara lote la Afrika lingekuwa mahala penye viongozi wenye imani za kidemokrasia. Kutokana na viongozi wengi kuyadumisha mamlaka yao kwa njia ya mabavu, Umoja wa Afrika mara nyingi unakaukiwa sauti.

Mkuu wa idara ya Afrika wa Deutsche Welle Claus Stäcker
Mkuu wa idara ya Afrika wa Deutsche Welle Claus StäckerPicha: DW

Mfano ni Mmenyekiti wa sasa wa Umoja huo ,Robert Mugabe wa Zimbabwe.Hakuna taasisi yoyote ya kiafrika iliyothubutu kuzizuia sera za Mugabe zinazoenda kinyume na misingi ya deomkrasia..

Rais Pierre Nkurunziza ni mshindi alieshindwa

Wapo viongozi watano barani Afrika, mashariki na magharibi mwa bara hilo wasiotaka kuondoka madarakani kwa hiari zao.Na Rais Nkurunziza wa Burundi ni miongoni mwa viongozi hao.

Mpaka sasa bado hajaweza kuzisoma alama za nyakati. Na licha ya kufanikiwa kurejea nyumbani baada ya jaribio la wanajeshi la kutaka kumwondoa madarakani, yeye bado hajawa mshindi.

Nukurunziza amewatishia wanasheria,wanasiasa na waandishi wa habari. Polisi wake wamewapiga risasi raia. Baada ya miaka 10 ya kuchukua hatua za busara katika kurejesha utulivu nchini, Nkurunziza amechapuka na kuicha njia ya maridhiano,ujenzi mpya wa nchi na kujenga demokrasia.

Rais Nkurunziza ameirudisha Burundi katika enzi za kijeshi. Amelijenga jeshi la vijana linalowatishia watu nchini, kwa niaba yake ili aweze kuhakikisha kwamba anachaguliwa tena. Vijana hao wanawatisha siyo tu washindani wa kisiasa bali pia wanavunja miiko: kwa kuwashutumu Watutsi kwa kula njama. Mvutano wa kikabila unaweza kuwa hatari kubwa sana kwa Burundi.

Njama hizo zinakumbusha yale yaliyotokea kati ya mwaka wa 1993 na 2000.Vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Hakuna njia nyingine nchini Burundi ila ile ya kusonga mbele na harakati za kuitekeleza katiba .Nkurunziza anaweza kuleta mabadiliko makubwa nchini Burundi ikiwa ataachana na mpango wa kuwania muhula wa tatu wa urais.

Mwandishi :Claus Stäcker.

Mfasiri:Mtullya Abdu.

Mhariri:Josephat Charo