1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri

26 Februari 2008

Wahariri wa magazeti watoa maoni juu ya miseto

https://p.dw.com/p/DDSS
Magazeti ya Ujerumani yakitoa maoni juu y kashfa ya kukwepa kodi.Picha: picture-alliance/ dpa

Wakati umebakia mwaka mmoja na nusu kabla ya uchaguzi mkuu kufanyika nchini Ujerumani vyama vya siasa vimo katika patashika ya kuunda miseto.

Wahariri wa magazeti wanatoa maoni yao juu ya patashika hizo.

Jee nani ashirikiane na nani katika kuunda serikali? Swali hilo lisingetokea thama na ujio wa nguvu wa chama cha mlengo wa kushoto-kwani chama cha Social demokratik kilichomo katika serikali ya mseto kinafikiria sana kushirikiana na chama hicho japo katika ngazi ya majimbo. Jambo hilo linaonekana kama kufuru kwa wengi nchini Ujerumani.

Lakini chama kingine kikuu, CDU kilichomo katika serikali ya mseto vilevile nacho kinafikiria kuunda mseto na chama cha kijani.

Gazeti la NORDBAYERISCHE KURIER linasema hakuna ubaya ikiwa chama hicho cha CDU kitashirikiana na chama cha kijani katika jimbo la Hamburg.

Lakini Mhariri wagazeti hilo pia anatilia maanani, ukweli kwamba chama cha mlengo wa kushoto cha wakomunisti wa zamani kimejijenga vizuri. Na kutokana na hayo mhariri wa gazeti la NORDBAYERISCHE anavitaka vyama vyote vifikirie upya.

Katika maoni yake gazeti la RHEIN- NECKER pia linasema, mseto baina ya CDU na chama cha kijani, litakuwa jambo la kuvutia katika siasa za Ujerumani.

Gazeti la HANDELSBLATT linakilaumu vikali chama cha Social Demokratik kwa kubadili nia juu ya chama cha mlengo wa kushoko -yaani chama cha wakomunisti wa zamani.

Gazeti linasema chama hicho kimo katika mkondo wa kujiharibia katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi septemba mwakani nchini Ujerumani.

Gazeti linasema msimamo wa sasa wa mwenyekiti wa chama cha Social Demokratik Kurt Beck utawafukuza wastahiki ambao katika mazingira mengine wangekipigia kura chama hicho. Na jambo baya zaidi, anasema mhariri ni iwapo mjumbe wa chama cha SPD Andrea Ypsilanti atatumia msaada wa kura za wakomunisti na wanaitikadi kali wa mlengo wa kushoto ili kuwa waziri mkuu wa jimbo la Hesse.

Lakini gazeti la ESSLINGER linasema,hayo yatasahauliwa haraka na wananchi.

Mhariri wa gazeti hilo anasema yumkini wastahiki wamebaini kuwa mwenyekiti wa chama cha Social Demokratik bwana Beck amevunja neno lake, lakini hasira za wapiga kura hao hazitadumu muda mrefu.

Gazeti linasema watu wamezoea kuwaona wanasiasa wakivunja ahadi zao.

Na kwa hakika watu hawajali ni chama gani kinashirikiana na nani. Muhimu kwao ni maudhui ya siasa.