1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mvutano waendelea Mashariki ya Kati

21 Oktoba 2015

Magazeti ya Ujerumani leo yanatoa maoni juu ya biashara ya silaha duniani, mvutano baina ya Waisraeli na Wapalestina na juu ya juhudi za kupambana na mabadiliko ya tabia nchi

https://p.dw.com/p/1GrQs
Wapalestina waandamana kusisitiza mshikamano
Wapalestina waandamana kusisitiza mshikamanoPicha: picture-alliance/dpa

Gazeti la "Märkische Oderzeitung" linasema mu sasa anaweza kuikosoa biashara ya silaha inayofanywa na Ujerumani kwa ujumla na pia kipengele kwa kipengele. Lakini mhariri wa gazeti hilo anatilia maanani kwamba mauzo ya silaha ndogo ndogo kutoka Ujerumani yamepungua Hata hivyo mhariri huyo anasema ni vigumu kudhibiti mauzo ya silaha za aina hiyo zinazotumika sana katika sehemu zenye migogoro.Mhariri huyo anaitaka jumuiya ya kimataifa isimame pamoja katika juhudi za kuzuia kuenea kwa silaha hizo.

Kuhusu biashara ya silaha duniani, gazeti la "Thüringer Allgemeine" linauliza iwapo dunia ingelikuwa na amani zaidi laiti Ujerumani isingeliuza silaha nje?

Mhariri wa gazeti hilo anasema mambo siyo rahisi kiasi hicho? Anasema kwa bahati mbaya zipo nchi nyingine zinazouza silaha vile vile. Gazeti la "Thüringer Allgemeine" anasema ikiwa mshindani yeyote anaacha pengo, basi litazibwa na Urusi au Marekani.

Ikiwa Ujerumani itaongoza katika juhudia za kuzuia biashara ya silaha, kama jinsi inavyoongoza katika kuushughulikia mgogoro wa wakimbizi, hilo lingekuwa jambo la sifa kubwa kwa Ujerumani.Lakini jee mwagizaji silaha gani ataliona hilo?

Gazeti la "Volksstimme" linauzungumzia mvutano baina ya Waisraeli na Wapalestina. Mhariri wa gazeti hilo anasema kutokana na vita vya nchini Syria kutiliwa maanani zaidi duniani,Wapalestina na Waisraeli wanapata mwanya wa kumalizina bila ya huruma.

Mhariri huyo anazitaka pande zote na hasa Marekani,Ujerumani na Umoja wa Ulaya zichukue hatua ili kuzuia umwagikaji wa damu wa kiwango kikubwa baina ya Israel na Wapalestina. Mhariri wa gazeti la "Volksstimme" anasema hatua hizo lazima zichukuliwe sasa hivi.

Mabavu hayatawasaidia Wapalestina

Nchi hizo zinapaswa kuingilia kati na kuwaambia Wapalestina kwamba hawataweza kuifikia shabaha yao kwa njia ya mabavu .Na katika upande mwingine anasema mhariri wa gazeti la "Volksstimme" kwamba lazima Israel iambiwe ifanye mabadiliko ya msingi katika siasa zake.

Gaza Demonstration Solidarität
Picha: Getty Images/AFP/M. Abed

Israel lazima iache mara moja siasa ya kuendelea na ujenzi wa makaazi ya walowezi wa kiyahudi kwenye Ukingo wa Magharibi na katika Jerusalem ya Mashariki.

Gazeti la "Eisenacher Presse" linatahadharisha juu ya hatari kubwa inayotokana na kuzidi kuharibika kwa mazingira

Mhariri wa gazeti hilo anasema Shirika la ushirikiano wa kiuchumi na maendeleo OECD limetoa mwito wa kufanya juhudi kubwa zaidi ili kupambana na hatari ya mabadiliko ya tabia nchi.

Mhariri wa "Eisenacher Presse" anatahadharisha kwamba juhudi hizo zinafanyika pole pole na mara nyingi zinarudi yuma. Anasema ndio sababu kwamba ni muhimu siyo tu kuzihimiza serikali na asasi za watetea mazingira, bali kila mwananchi anapaswa kushirikishwa katika juhudi za kupambana na mabadiliko ya hali ya hewa.

Mwandishi:Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri: