1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni: Mtazamo wa majonzi katika mto Nile

Ursula Kissel8 Julai 2013

Mapinduzi yaliyofanywa na jeshi nchini Misri yalifanywa kwa busara lakini hii haimaanishi kuwa yalikuwa halali, na wala siyo mapinduzi ya pili kama wanavyodai wapinzani wa Mursi, anasema Mwandishi wa DW Mudhoon Loay.

https://p.dw.com/p/193ez

Bila shaka mapinduzi yaliyofanywa na waziri wa ulinzi ambae pia ni mkuu wa majeshi ya nchi hiyo Abdel Fatah al-Sisi yalifanyika kwa busara. Al-Sisi alitangaza mapinduzi hayo, na kisha kusitisha katiba akiwa pamoja na viongozi wakuu wa dini - Shehe mkuu wa Chuo Kikuu cha Azhar, Ahmed al-Tajjib papa wa madhehebu ya Koptik, Tawadros II, mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel Mohamed Elbaradei pamoja na wawakilishi wa vuguvugu la Tamarod lililoongoza maandamano dhidi ya Mursi. Hata hivyo, busara hii haiwezi kuficha ukweli kwamba haya yalikuwa mapinduzi dhidi ya rais aliechaguliwa kidemokrasia katika tukio hilo la hatari na la kipekee. Na wala si mapinduzi ya pili kama wanavyodai wapinzani wa Mursi.

Mwandishi wa DW, Loay Mudhoon.
Mwandishi wa DW, Loay Mudhoon.Picha: DW

Mapinduzi yalikuwa yanaepukika

Magogoro wa madaraka kati ya vyama vya Kiislamu na waliberali haukuamuliwa kutokana na ufanisi wa uhamasishaji wa maandamano ya Juni 30, bali na uingiliaji kati wa jeshi. Leo tunajua kuwa uamuzi wa jeshi kumpindua rais Mursi ulichukuliwa siku moja kabla ya kuanza kwa maandamano hayo. Pia ushiriki wa chama cha kisalafi cha An-Nour kama mwakilishi wa vyama vinavyofuata siasa za dini katika hafla ya kijeshi ya upokonyaji madaraka hakuwezi kubadili ukweli. Kwa sababu hii yafaa kuelezea kilichofanywa na jeshi kwa maneno sahihi: Ni mapinduzi haramu na pigo kwa mchakato wa demokrasia.

Hakuna shaka kwamba Mursi alishindwa kuitawala nchi hiyo kubwa kabisaa katika ulimwengu wa kiarabu. Juu ya yote, alishindwa vibaya katika mchakato wa kuunganisha nchi iliyogawika kisiasa na kuwa rais wa Wamisri wote. Hili lilikuwa muhimu sana kwa kuzingatia ukweli kuwa alichaguliwa kwa wingi mdogo mwaka mmoja uliyopita. Pia kikubwa kilikuwa kushindwa kwa serikali yake kushughulikia matatizo makubwa ya kiuchumi yaliyowasababishia mateso makubwa raia. Serikali yake ilifanya kidogo kushughulikia matatizo ya ukosefu wa ajira, mfumuko wa bei na uhaba wa mafuta. Lakini je, uingiliaji wa jeshi ulikuwa muhimu kufupisha muhula wa Mursi? Ikizingatiwa kuwa mamlaka ya iliondolewa kabisaa kufuatia maandamano makubwa dhidi yake, mtu anatilia shaka mapinduzi hayo.

Muungano wa mashaka dhidi ya Mursi

Ni dhahiri tayari, kwamba muungano wa upinzani dhidi ya Mursi umekosa fursa ya kihistoria, ya kuufanya Udugu wa kiislamu, ambao ndiyo watetezi wa Uislamu kushindwa kisiasa. Badala yake wamewapa fursa nyingine ya kuandika hadhithi ya mashahidi. Kufuatia uzoefu wa nchini Algeria mwaka 1992 ambapo majenerali walifanya mapinduzi na kukipokonya ushindi chama cha Kiislamu cha Islamic Salvation Front, na sasa hiki kilichofanyika mjini Cairo, vyama vikuu vya Kiislamu vinapata sababu ya kuamini kuwa kila vinaposhinda uchaguzi wa kidemokrasia, vinahujumiwa au serikali zake kupinduliwa.

Kuna mashaka pia iwapo wapinzani wa Mursi waliogawanyika wangeweza kuwa na msimamo mmoja wa kisiasa dhidi ya vyama vya Kiislamu. Kukataa kwao kufanya majadiliano ya rais huyo wa zamani na tangazo lao la kususia uchaguzi wa bunge vilizidisha tu mkwano. Pia kuungana kwao na masalia ya utawala wa rais wa zamani Hosni Mubarak kunaacha maswali juu ya nia yao hasa.

Licha ya hayo, kama muungano huo unaompinga Mursi unaamini kuwa jeshi liliingilia kati kutekeleza matakwa ya raia na kusimamia demokrasia, basi wanafikiri kama washamba. Kwa sababu majenerali hao wanachofikiria kwanza ni kulinda maslahi yao. Jeshi la Misri linajulikana kwa rushwa iliyokithiri na linadhibiti si chini ya robo ya uchumi wa Misri. Juu ya hayo, limeshindwa kabisaa kusimamia miaka miwili ya kwanza, baada ya kuondoka kwa Hosni Mubarak.

Kuondolewa kwa nguvu rais Mohamed Mursi si tu kumeongeza mgawanyiko nchini Misri, lakini pia kunaitishia nchi hiyo yenye wakazi milioni 90 kutotawalika na kuisogeza karibu katika kingo za kuanguka. Ili kuzuia hali hii isitokee, makundi yote ya kisiasa yanapawa kushirikishwa katika mchakato wa kisiasa, hasa kundi la Udugu wa Kiislamu kwa sababu linaendelea kuwa kundi lililojipanga vizuri zaidi nchini humo. Majaribio yote ya kuanzisha utaratibu mpya baada ya Mursi pasipo kuwashirikisha wao yatakuwa na nafasi ndogo sana ya kufanikiwa.

Ujerumani na mataifa ya Ulaya yanapaswa kuutaka utawala nchini humo kuacha mara moja kufanya ukandamizaji dhidi ya Udugu wa Kiislamu na viongozi wake na walitake jeshi kuheshimu ahadi yake ya kuandika katiba mpya na kufanya uchaguzi haraka iwezekanvyo.