1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni: Bolton ni kizingiti cha makubaliano ya Iran

Saumu Mwasimba
23 Machi 2018

Hatua ya rais Trump ya kumteua John Bolton kuwa mshauri wa masuala ya usalama wa kitaifa imechochea kujitokeza hisia kali duniani. Wadadisi wanahisi ni msumari mwingine katika jeneza la kuyazika makubaliano ya Iran

https://p.dw.com/p/2urpJ
USA John Bolton
Picha: picture-alliance/AP Photo/A. Adams

H.R.McMaster jenerali wa ngazi ya juu wa nyota tatu amepata fursa ya kukaa kwa zaidi ya mwaka mmoja katika serikali ya rais Donald Trump. Huo ni muda wa kutosha uliovunja rekodi kwa mtu yoyote ambaye sio jamaa yake Trump kuwahi kufanya kazi katika ikulu ya rais huyo. Mtangulizi wake Michael Flynn ambaye vile vile ni afisa wa zamani wa jeshi alipata fursa ya kufanya kazi White House kwa kipindi cha chini ya mwezi mmoja tu na baadaye akaungama kosa la kuidanganya FBI shirika la upepelezi la Marekani kuhusu kuwa na mawasiliano na serikali ya Urusi kama sehemu ya uchunguzi ulioko chini ya jopo maalum linaloongozwa na Robert Muller.

Lakini wakati waziri wa mambo ya nje aliyetimuliwa Rex Tillerson alipoaga rasmi wizara ya mambo ya nje siku ya Jumatano, Uhusiano binafsi wa McMaster na rais Trump ambao ndio uliomfanya aendelee kuwepo Ikulu ulisemekana kuwa umeshaingia mashakani, kama toka hapo uliwahi kuwepo. Kutoelewana kwa Trump na McMaster kuliripotiwa kwamba sio tu kulitokana na mtindo wa rais huyo anavyoyaendesha mambo lakini hata kuhusu utiaji saini wa masuala kama yanayohusiana na Iran na Urusi. MacMaster  alihoji dhidi ya kuyafuta makubaliano na Iran na kuchukua msimamo mkali dhidi ya Urusi.

Kauli ya jenerali huyo hivi karibuni katika mkutano wa usalama uliofanyika mjini Munich, kwamba Urusi bila shaka yoyote iliingilia uchaguzi wa Marekani, ilimfanya kukosolewa vikali na bosi wake kupitia mtandao wa kijamii wa Twita na si ajabu kwamba hapo ndipo palipoanzia mwisho wa safari yake katika wadhifa aliokuwa nao. Sio siri kwamba wengi nchini Marekani watamkumbuka ikiwemo wabunge wa Marekani na wanadiplomasia wa nje waliokuwa wakimtazama kama afisa wa kuaminiwa na mshirika wa kuweza kuzungumza naye pamoja na kwamba alikuwa ni kama ndege anayewindwa.

Michael Knigge Kommentarbild App
Mwandishi wa DW:Michael Knigge

Kama alivyokuwa mrithi wake John Bolton, McMaster alibaini hadharani juu ya kufikiria kile alichokiita kuwa shambulizi la kujikinga  dhidi ya Korea Kaskazini. Lakini tafauti na Bolton, McMaster hakuwahi kuangaliwa kama mtu asiyejali au mpigia debe vita. Sifa ya Bolton inafahamika, alikuwa ni mmoja kati ya waungaji mkono na wafuasi wakubwa wa uamuzi wa rais wa zamani wa Marekani Goerge W Bush wa kuivamia Iraq.

Kipindi kifupi alichokuwa kama balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, nafasi ambayo hakuwahi hata kuthibitishwa na baraza la senete la Marekani, kiliandamwa na sauti za ukosowaji wake wa wazi wazi kuelekea chombo hicho, na kwa kuangalia maoni yaliyochapishwa mwezi Desemba katika jarida la Wall Street Journal la Marekani yaliyokuwa na kichwa cha maneno kilichosema ''Jinsi ya kuuzuia Umoja wa Mataifa kutoendelea kupokea fedha'' basi hapana shaka msimamo wa Bolton haujabadilika.

Kuhusu Iran Bolton amekuwa akizungumzia mtazamo ule ule wa matumizi ya nguvu dhidi ya nchi hiyo kama ambavyo alikuwa akiunga mkono kuivamia Iraq. Na juu ya hilo mara kadhaa ameripotiwa kwamba ameshawhi kutowa mwito wa kufanyika mageuzi ya uongozi nchini Iran. Na kama haitoshi gazeti la New York Times limeshawahi kuripoti miaka mitatu iliyopita kwamba Bolton aliwahi kusema kwamba ili kuizuia Iran isitengeneze bomu ni lazima nchi hiyo iripuliwe kwa bomu.

Pamoja na kwamba Marekani imeanza rasmi msimu wa machipuko kwa kuzuka vita vya kibiashara na China na uteuzi huu wa Bolton kila mmoja anajihisi kama ndo kwanza msimu wa baridi kali umewavamia.

Mwandishi.Michael Knigge/Saumu Mwasimba

Mhariri:Jopsehat Charo