1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazetini Ujerumani

P.Martin10 Februari 2009

Kuteuliwa kwa Waziri mpya wa Uchumi wa Ujerumani mara nyingine tena ni mada iliyogonga vichwa vya habari katika magazeti ya Ujerumani leo Jumanne.

https://p.dw.com/p/Gqks

Uchaguzi wa Israel pia umeshughulikiwa na magazeti mengi ya Ujerumani.Basi tukianza na uchaguzi huo gazeti la WESTFALLEN BLATT linasema:

Huo si uchaguzi fulani tu katika nchi kadhaa kwani maendeleo ya muda mfupi katika kanda ya Mashariki ya Kati yanategemea matokeo ya uchaguzi huo.Mgogoro wa Gaza na mradi wa nyuklia wa Iran ni mada kuu katika uchaguzi wa leo nchini Israel.Kwa hivyo,si jambo la kushangaza kuona wapiga kura wakivutiwa na viongozi wanachochea misimamo mikali dhidi ya Wapalestina na Iran laendelea gazeti la WESTFALLEN BLATT.

Na kuhusu Waziri mpya wa Uchumi wa Ujerumani Karl-Theodor zu Guttenberg anaeshika rasmi wadhifa wake leo hii,gazeti la FRANKFURTER ALLGEMEINE ZEITUNG linasema:

Licha ya kuwepo mashaka,hilo ni suluhisho pekee lililoweza kutolewa na mwenyekiti wa chama cha CSU Horst Seehofer. Likiendelea gazeti hilo linasema,zu Guttenberg hana muda wa kuthibitisha ikiwa kweli amependezwa na wadhifa aliopewa.Yeye ni mgeni katika sera za uchumi hata ikiwa ujuzi aliopata katika kampuni za familia yake na katika bodi ya usimamizi huenda ukamsaidia.

Gazeti la BRAUNSCHWEIGER ZEITUNG likigusia mada hiyo linaeleza hivi:

Serikali ya Shirikisho la Ujerumani haipaswi kuwa kama ni uwanja wa mazoezi kwa vichipukizi wa kisiasa kutoka jimbo la Bavaria.Kwa maoni ya gazeti hilo,kuna walakini fulani katika uhusiano wa CSU na vyama vingine katika serikali ya mseto.Hata chama cha CDU kimeathirika.Kwani chama hicho hakijatumia fursa iliyotokana na kujiuzulu kwa Michael Glos. Chama hicho kingeweza kuthibitisha kuwa kina wajuzi wake wa uchumi na hiyo ingekuwa ishara nzuri kwa wapiga kura wanaokimbilia chama cha kiliberali cha FDP.Kwa hivyo Kansela aache kumtetea Mwenyekiti wa CSU Horst Seehofer.

Tukibadili mada tunaligeukia gazeti la RHEINISCHE POST linalosema:

Waziri Mkuu wa Jimbo la Niedersachsen Christian Wullf amemtuhumu Waziri wa Fedha wa Ujerumani Peer Steinbrück kuwa mkakati wa kuokoa uchumi wa waziri huyo si barabara. Anasema, kusifanywe kosa la kuingilia kiini cha uchumi kwa kutaifisha baadhi ya mashirika ya fedha.Kwa maoni ya Wullf serikali haina ujuzi bora zaidi wa kiuchumi kuongoza benki na mashirika ya fedha.