1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maelfu wapiga kura ya maoni Kusini mwa Sudan

9 Januari 2011

Wananchi wa Sudan ya Kusini wameanza kupiga kura ya maoni leo hii ambayo inatarajiwa sana kuamua kujitenga na Sudan ya kaskazini.

https://p.dw.com/p/zvWZ
Mkaazi wa Sudan Kusini akibeba bendera ya eneo laoPicha: picture alliance/dpa

Kura hiyo ya maoni ya juma moja ni kipengele muhimu cha makubaliano ya amani ya mwaka 2005 ambayo yamekomesha vita vya wenyewe kwa wenyewe kati ya Waislamu wa kaskazini ya Sudan na Wakristo wa kusini ambavyo vimeuwa watu milioni mbili na kuwapotozea makaazi zaidi ya watu milioni nne.

Kipengee muhimu

Rais wa Sudan kusini Salva Kiir akizuwia machozi yasimtoke wakati wa kupiga kura alitowa heshima zake kwa kiongozi wa zamani wa waasi John Garang ambaye ameuwawa katika ajali ya helikopta hapo mwaka 2005 pamoja na watu wengine waliopoteza maisha yao katika vita.

Muda mfupi baada ya kupiga kura yake katika mji mkuu wa Juba amesema kwamba anaamini Dr. Garang na wale waliokufa pamoja naye watakuwa hawakufa bure.

Kwa Salva Kiir leo ilikuwa ni siku ya kihistoria kwa watu wake.

Watu milioni nne

NO FLASH Wahlen im Sudan
Wafuasi wa Salva Kiir ,rais wa eneo la Kusini mwa SudanPicha: picture-alliance/dpa

Watu wanaokaribia milioni nne wa kusini wamejiandikisha kupiga kura hiyo ambayo inatakiwa asilimia 60 ya wapiga kura wake washiriki kupiga kura ili iweze kuwa imefanikiwa.

Wengi wanatarajia kuwa wananchi wa Sudan ya kusini watachagua kujitenga na Sudan kusini.

Kulikuwa na misururu mirefu katika vituo vya kupiga kura katika eneo zima la mji wa Juba leo hii na mamia ya watu walilala katika vituo vya kupigia kura katika kituo cha kumbukumbu cha Garang.

Wakati wananchi wa kusini wamejitokeza kwa wingi kupiga kura wale waliojitokeza katika mji mkuu wa Khartoum hawakuwa wengi katika siku hiyo ya kwanza ya kupiga kura.

Hisia za Kaskazini

Wakati wananchi wa kaskazini mwa Sudan hawafurahii kura hiyo kwa kutambua kwamba itaigawa Sudan baadhi ya wananchi wa kusini walioko Khartoum pia wanahisi kwamba watafanywa kuwa wageni huko kaskazini iwapo kusini itajitenga na kaskazini.

Kiongozi mwandamizi wa Sudan kusini leo hii ameionya serikali ya Sudan kaskazini kuheshimu makubaliano juu ya wilaya ya Abyei baada ya kuzuka upya kwa mapigano katika eneo hilo ambapo watu kadhaa waliuwawa na kujeruhiwa hapo jana.

NO FLASH Sudan Referendum
Wanaharakati wanaotaka Sudan ya kusini ijitenge:Sudan ya Kaskazini ina hisia tofautiPicha: AP

Kura hiyo ya maoni ambapo watu wengi walikuwa na wasiwasi iwapo itaweza kufanyika kwa wakati uliopangwa imezusha hofu ya kuibuka upya kwa mzozo kati ya kusini na kaskazini likiwemo suala la Abyei yenye utajiri wa mafuta ambayo inabidi iamuwe iwapo inajiunga na Sudan kaskazini au kusini.

Masuala mengi hayajapatiwa ufumbuzi ikiwemo mipaka ya maeneo yenye akiba kubwa ya mafuta yalioko kusini mwa Sudan.

Mwandishi: Mohamed Dahman

Mhariri: Josephat Charo