1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maelfu waandamana kupinga ukatili wa polisi

Sudi Mnette
7 Juni 2020

Katika kile kinachoelezwa kuwa ni maandamano makubwa zaidi kushuhudiwa, dhidi ya ukatili wa polisi na ubaguzi wa rangi, maelfu ya waandamanaji wameshiriki Marekani na maeneo mengine ya ulimwengu.

https://p.dw.com/p/3dNub
USA | Washington | Black Lives Matter Protest
Picha: Getty Images/C. Somodevilla

Makamo wa rais wa zamani wa Marekani Joe Biden ametumia mwanya huo kujipigia chapuo kisiasa kwa kutetea mabadiliko ya muundo wa jeshi la polisi kwa kile alichokiita hatua muafaka ya muda mrefu, sera kamili ya kubadili ubaguzi wa kimfumo. Endapo atachaguliwa katika uchaguzi wa Novemba.

Kupitia gazeti la kila siku la mjini Los Angeles, Los Angeles Times, amesema kama atachaguliwa ataunda kamisheni ya polisi ya taifa itakayoshughulikia masuala hayo ndani ya siku 100 akiwa ofisini.

Maafisa wawili wa polisi wa Buffalo wameshitakiwa

USA | New York | Black Lives Matter Protest
Maandamano ya kupinga unyanyasaji New YorkPicha: Getty Images/B. Bennette

Wakati hayo yanaelezwa maafisa wawili wa polisi  katika jiji la Buffalo, katika jimbo la New York wameshitakiwa kwa kufanya shambulizi, baada ya kuonekana katika video wakimsukuma mwandamanaji mzee wa umri wa miaka 75, wakati wa maandamano ya kupinga mauwaji ya Katika video hiyo, mzee huyo alionekana akianguka chini, kichwa chake kujigonga katika lami, akapoteza fahamu na kuanza kuvuja damu.

Katika mji wa kaskazini/magharibi wa Marekani wa Seattle, kumeshuhudiwa maandamano ya siku ya tisa mfululizo, kufuatia kifo cha Floyd. Kundi kubwa la wafanyakazi wa sekta ya afya, na wengi wao wakiwa wamevaa mavazi ya maabara wameshiriki maandamano hayo. Mwanadamaji mmoja alibeba bango lilioandikwa "Wauguzi wanapiga magoti nawe, sio kukupigia wewe." Na mwengine "Ukatili wa polisi na ubaguzi ni dharura ya afya ya umma."

Waandamanaji wapuuza marufu ya kutoka nje New York

Waandamanaji pia walijitokeza mjini New York, pamoja na wasiwasi kati ya polisi na waandamanaji kutokana na marufuku ya mamlaka ya jiji hilo ya kutotoka nje nyakati za jioni. Mikusanyiko imefanyika siku nzima na jioni katika maeneo ya Manhattan, Brooklyn na Bronx. Wanasiasa wa watetezi wa haki za kiraia walijitokeza kuipinga marufuku iliyowekwa wakisema itasababisha makabiliano makali kati ya polisi na raia.

Kadhalika waandamanaji wajitokeza katika viunga vya jiji la Washington, ambalo limekuwa na maandamano ya kila siku tangu juma lililopita. Idadi ya watu kwa maandamano hayo inakadiriwa kuwa kubwa kuliko maandamano yoyote ya kupinga ukatili wa polisi yaliowahi kufanyika katika jiji hilo tangu kuuwawa kwa George Floyd.

Ujerumani na Uingereza pia watu wamejitokeza kuunga mkono maandamano hayo. Kwa Ujerumani watu wamekusanyika Cologne, Münster na Nuremberg lakini pia kumeonekana makundi makubwa katika maeneo ya miji midogo kama Flensburg huko katika jimbo la kaskazini la Schleswig-Holstein. Nchini Uingereza katika jiji la London, Korea Kusini, Seoul pamoja na miji mingine duniani.

Chanzo: DW