1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MADRID: Rais wa zamani wa Argentina, Bibi Isabel Peron aachiwa huru kwa muda nchini Uhispania.

13 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCax

Maafisa wa Uhispania wamemwachia huru kwa muda rais wa zamani wa Argentina Isabel Peron aliyetiwa nguvu jana nyumbani kwake mjini Madrid.

Jaji wa Argentina aliagiza rais huyo wa zamani akamatwe kutokana na kutoweka mwanaharakati wa mrengo wa kushoto miaka ya sabini.

Bi Isabel Peron pia anachunguzwa na hakimu mwengine wa Argentina kwa uhusiano wake na makundi ya mrengo wa kulia ya wakereketwa wanaotuhumiwa kuwaua watu takriban elfu moja na mia tano.

Serikali ya Argentina sasa ina muda wa siku arobaini kuwasilisha maombi ya kutaka rais huyo wa zamani arejeshwe kwao.

Bi Isabel Peron mwenye umri wa miaka sabini na mitano aliingia madarakani mwaka elfu moja, mia tisa na sabini na nne baada ya kifo cha rais wa wakati huo Juan Peron ambaye alikuwa mumewe.

Serikali ya Bi Peron ilipinduliwa mwaka wa elfu moja mia tisa na sabini na sita na amekuwa akiishi uhamishoni nchini Uhispania tangu mwaka elfu moja mia tisa na themanini na moja.