1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandamano yanaendelea kwa siku ya tatu Bahrein

16 Februari 2011

Maelfu wa washia wakishawishiwa na wimbi la mageuzi nchini Tunisia na Misri,wamejikusanya hii leo kati kati ya mji mkuu wa Bahrein- Manama,kuomboleza kifo cha mmoja wapo wa wenzao walioangukia mhanga wa machafuko.

https://p.dw.com/p/10Hnj
Waandamanaji wako katika uwanja wa LuluPicha: AP

Bwana huyo aliuliwa jana wakati wa maziko ya kijana mwengine aliyeuwawa jumatatu iliyopita akiwa na umri wa miaka 22.

Kwa mujibu wa mashahidi waandamanaji wasiopungua elfu mbili walikesha jana usiku katika kambi ya mahema waliyoipiga katika njia panda ijulikanayo kama"Lulu".

Polisi wamejiweka kando na wizara ya mambo ya ndani imesema shughuli za usafiri zitaendelea kama kawaida.

Katika hotuba yake kwa njia ya televisheni,mfalme Hamad ben Issa al Khalifa alitoa rambi rambi zake kwa familia za vijana hao wawili na kuahidi tume maalum itaundwa kuchunguza kilichopelekea vijana hao kuuwawa.

Bahrain Unruhen Proteste
Wakinamama wa Bahrein nao pia wanaandamanaPicha: dapd

Wengi wa wananchi wa Bahrein ni wa madhehebu ya Shia lakini familia ya kifalme inayotawala ni ya madhehebu ya sunni.Waandamanaji wa kishia wanalalamika wanabaguliwa wanapohitaji nyumba,huduma za afya au ajira katika mashirika yanayoongozwa na serikali.

Mwenyekiti wa shirika la haki za binaadam la Bahrein Nabil Rajab anasema sababu zinazowafanya watu wateremke majiani:

"Sio kuuangusha utawala.Wanataka haki za binaadam na uhuru wa kutoa maoni yao.Wanataka mateso yakome- na kinyume na Misri,hunchini Bahrein hakuna anaetaka kuwang'owa madarakani watawala."

Hata hivyo waandamanaji wanadai ajiuzulu waziri mkuu Khalifa ben Salman al Khalifa anaeitawala nchi hiyo tangu uhuru mwaka 1971.Wanashinikiza pia waachiwe huru wafungwa wa kisiasa-jambo ambalo serikali imelikubali na itungwe katiba mpya pia.

Barack Obama
Rais Barack Obama wa MarekaniPicha: AP

Marekani imeelezea wasi wasi kufuatia machafuko yanayoitikisa nchi hiyo ndogo ya kifalme katika ghuba kunakokutikana kituo cha jeshi la wanamaji la Marekani.Bahrein ni kituo muhimu pia cha shughuli za fedha katika eneo hilo.

Chama kikuu cha upinzani cha washiya-Wefaq,kilichoamua kusitisha shughuli zake bungeni,kimesema kinapanga kuzungumza na serikali hii leo.

Serikali ya Bahrein imetangaza kutenga dala milioni 417 kugharimia huduma za jamii ikiwa ni pamoja na ruzuku kwa bidhaa muhimu kwa jamii.

Kinyume na nchi nyengine za Ghuba,Bahrein ambayo nusu ya wakaazi wake milioni moja na laki tatu ni wahamiaji,haina rasli mali kubwa hivyo.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Reuters,afp

Mpitiaji:Abdul-Rahman