1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandamano ya wanawake dhidi ya Trump

Sekione Kitojo
22 Januari 2017

Wanawake walimiminika mjini Washington Jumamosi (21.01.2017)kuelezea wasi wasi wao, hasira baada ya Donald Trump kuingia madarakani nchini Marekani akiwa rais wa 45, katika "maandamano ya wanawake mjini Washington.

https://p.dw.com/p/2WCjn
Washington Women's March Trump Proteste
Wanawake kutoka sehemu mbali mbali wakiandamana mjini WashingtonPicha: DW/M. Shwayder

Maandamano hayo yamewahamasisha  wengi  katika  taifa  hilo, na wengine zaidi  ya  milioni  moja  wakimiminika  katika  mitaa ya  miji ya  Marekani wakiandamana  kwa  amani. Maandamano  hayo  ni ishara  ya  awali  ya  upinzani  mkali  anaokabiliana  nao  rais  huyo kutoka  chama  cha  Republican.

Washington Women's March Trump Proteste
Wanawake wakiandamana dhidi ya Trump mjini WashingtonPicha: DW/M. Shwayder

Mamia  kwa  maelfu  ya  wanawake , wengi  wakivalia kofia za  rangi ya  waridi , pinki kupinga matamshi ya  Trump  ambayo  yamezusha hasira  miongoni  mwa  wanawake, walijazana  mjini  Washington karibu  na  Ikulu  ya  Marekani  ya  White House.

Mamia  kwa  maelfu  ya  wanawake  waliingia  mitaani  mjini New York, Los Angeles , Chicago na Boston kumdhihaki Trump katika siku yake kamili ya kuwapo madarakani.

Mkusanyiko wa watu walioandamana mjini Washington ulionekana kuwa mkubwa  zaidi  ya  kundi  lililojitokeza  katika  sherehe  za kuapishwa  kwa  Trump.

Wanawake waandamana duniani kote

Duniani  kote  pia  wanawake  waliandamana  wakiwaunga  mkono wanawake  wa  Marekani  na waliungana  kuonesha  hasira  yao katika  miji  mingi, na  kufikisha  idadi   ya  waliohudhuria maandamano  hayo  kufikia   zaidi  ya  wanawake  milioni  4, wamesema  watayarishaji  wa  maandamano  hayo.

Rais  wa  Marekani  Donald Trump  anatarajia  kukutana  na  waziri mkuu  wa  Uingereza  Theresa May pamoja  na  rais  wa  Mexico Enrique ena Nieto , washirika  wa  muda  mrefu  wa  Marekani  hivi karibuni , wakiwa  na  wasi  wasi  juu  ya  vipi uongozi  wake unaweza  kuathiri uhusiano  wao  na  Marekani.

London Premierministerin Theresa May bei Rede zu Brexit
Waziri mkuu wa Uingereza Theresa MayPicha: Getty Images/K. Wigglesworth

Trump  atakutana  siku  ya  Ijumaa  na  May  mjini  Washington , amesema  msemaji  wa  Ikulu  ya  Marekani  ya  White House Sean Spicer jana  Jumamosi.

Mkutano  wao  utakuwa  fursa  kwa  May, ambaye  hapo kabla alipata  taabu  ya  kujenga  uhusiano na  kikosi  cha  Trump cha kipindi  cha  mpito, kujadili  kile  ambacho  kwa  muda  mrefu kilielezwa  kuwa  ni "uhusiano  maalum" kati  ya  mataifa  hayo mawili, nguzo muhimu  ya  sera  za  kigeni  za  Uingereza.

Trump aliidhinisha Uingereza kujitoa EU

Trump , ambaye  aliidhinisha  kura  ya  Uingereza  kujitoa  kutoka Umoja  wa  ulaya  na  ni  rafiki  wa  mkosoaji  mkubwa  wa  May Nigel Farage , amesema  anataka  kutayarisha  makubaliano  ya  haraka ya  kibishara  kati  ya  mataifa  hayo  mawili  , Marekani  na Uingereza.

Biashara  itakuwa  pia  ajenda  katika  mkutano  kati  ya  Trump  na Pena Nieto  pamoja  na  usalama  na  uhamiaji, Spicer aliwaambia waandishi  habari.

Enrique Pena Nieto und Donald Trump
Rais wa Mexico Enrique Pena Nieto alipokutana na rais wa Marekani Trump kabla ya kuapishwa Agosti 31.08.2016Picha: picture-alliance/AP Photo/D. Lopez-Mills

Baada  ya  kuapishwa  rais Donald Trump  kuwa  rais  wa  45  nchini Marekani , "dunia ya  kale  ya  karne  ya  20 haipo  tena," waziri  wa mambo  ya  kigeni  wa  Ujerumani  Frank-Walter Steinmeier aliandika  katika  makala  maalum  kwa  ajili  ya  gazeti  la  Bild am Sonntag leo  Jumapili (22.01.2017).

Vipi  dunia  ya  kesho itakavyoonekana  hilo  halijaamuliwa , bado hilo  liko  wazi," ameongeza  waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa Ujerumani. "Kama  kawaida  wakati  madaraka  yanatoka  kutoka mkono  mmoja  kwenda  mwingine , kunakuwa  na  hali  ya sintofahamu, wasi  wasi  na  maswali juu  ya  mwelekeo  wa  uongozi mpya.  Lakini  katika  nyakati  hizi  za mkanganyiko  mpya  wa  dunia, leo hii  kuna  mambo mengi  yanayohitajika," amesema  Steinmeier.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / rtre / afpe

Mhariri: Yusra Buwayhid