1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maandamano Iran kuunga mkono utawala

Sekione Kitojo
3 Januari 2018

Maelfu ya watu waliandamana katika miji mbali mbali nchini Iran, katika hatua ya kuonesha uimara wa utawala baada ya siku kadhaa  za machafuko na televisheni ya taifa ilionesha watu wengi wakiandamana katika miji kadhaa.

https://p.dw.com/p/2qGHO
Iran Teheran Jahrestag Islamische Revolution Anti US Demo
Picha: Reuters/Iran Presidency

Watu  walikuwa  wakipiga  makelele , "kiongozi, tuko tayari"  na  picha  zilionesha  maelfu  ya  watu wakiandamana  katika  miji  ya  Ahvaz, Kermanshah, Gorgan  na  kwingineko.  Waandamanaji  walipunga bendera  ya  Iran  na  picha  za  kiongozi  mkuu  wa kidini Ayatollah Ali Khamenei , pamoja  na  mabango yaliyoandikwa , "kifo  kwa wachochezi".

Gegner der Atomverhandlung in Iran
Maandamano mjini Tehran Picha: Isna

"Tutatoa  damu  katika  mishipa  yetu  kwa  kiongozi  wetu," ilikuwa  ni  kauli  mbiu  nyingine  waandamanaji waliyokuwa  wakiimba.  Kumekuwa  na  ripoti  chache  za maandamano  ya  kuipinga  serikali  baada  ya utawala kuja  pamoja  kupambana  na  ghasia  hizo  wiki  iliyopita ambapo  watu  kiasi  ya  21  waliouwawa.

Marekani  iliendelea  kuweka  mbinyo kwa  viongozi wa taifa  hilo  la  Kiislamu, ambapo balozi  wa  Marekani  katika Umoja  wa  Mataifa  Nikki Haley akitoa wito  kwa  Umoja huo  kufanya  kikao cha  dharura  kuzungumzia  hali  hiyo.

"Watu  wa  Iran  wanalilia  uhuru," amesema  katika mkutano  na  waandishi  habari. "Watu  wote  wanaopenda kuwa huru   wanapaswa  kusimama kuwaunga  mkono." amesema  Haley.

Nikki Haley
Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Nikki HaleyPicha: picture-alliance/M.Altaffer

Mataifa mengi yanaangalia 

Msemaji  wa  wizara  ya  mambo  ya  kigeni  ya  Marekani Heather  Nauert  alisema  kwamba  mataifa  yote yanaangalia  kwa  karibu  hali  nchini  Iran.

„Mataifa  mengi duniani yanaangalia kile kinachotokea Iran, wanaangalia kwa karibu sana. Marekani , hata  washirika  wetu na marafiki  pia  wanaangalia. Ufaransa , Ujerumani, Uingereza, mmesikia  mengi  kutoka  kwao  katika  siku  za  hivi  karibuni wakielezea  wasi  wasi  wao, kama  tulivyoeleza wasi wasi  wetu juu  ya  ukandamizaji dhidi  ya  haki  za  binadamu. Tunaangalia hayo  kwa  karibu. Hii  ni  pamoja  na  kukamatwa watu kwa kuandamana  kwa  amani."

Viongozi  wa  Iran wamesema  maandamano , ambayo yalianza  kuhusiana  na  suala  ya  kiuchumi  Disemba  28 lakini  haraka  yakageuka  kuwa  makubwa  zaidi, walikuwa sehemu  ya  mpango  wa   mataifa  ya  kigeni kuudhoofisha utawala  huo. "Maadui   wamejiunga  pamoja na  wanatumia  kila  mbinu , fedha , silaha , sera  na huduma za  ujasusi  kuleta  matatizo  katika  taifa  hilo  la Kiislamu, amesema  Ali  Khamenei.

Iran, Tehran, Ayatollah Ali Khamanei
Kiongozi mkuu wa kidini nchini Iran Ayatollah Ali KhameneiPicha: picture-alliance

Hata wanamageuzi , ambao  waliunga  mkono maandamano  makubwa  yaliyopita dhidi  ya  madai  ya udanganyifu  katika  uchaguzi  mwaka  2009 , mara  hii wameshutumu  ghasia  na  uungaji  mkono  uliopata kutoka  Marekani.

Mwandishi. Sekione  Kitojo / afpe

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman