1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

LONDON: Balozi wa Iran aitaka Uingereza ionyeshe ukarimu

7 Aprili 2007
https://p.dw.com/p/CCBl

Balozi wa Iran nchini Uingereza, Rasoul Movahedian, ameitaka Uingereza ionyeshe ukarimu baada ya Iran kuwaachilia huru wanamamaji 15 waliokuwa wakizuiliwa mjini Tehran.

Matamshi ya balozi huyo yanafuatia madai yaliyotolewa na mabaharia wa Uingereza katika mkutano na waandishi wa habari mjini London kwamba walikamatwa wakati walipokuwa katika eneo la bahari la Irak na wala sio katika himaya ya Iran.

Walisema walikuwa wakifanya operesheni yao ya kawaida wakati walipozingirwa na wanajeshi wa Iran na kutekwa na haikuwa jambo la busara kupambana nao kwa wakati huo. Aidha wanamaji hao walisema kila mtu alizuiliwa katika chumba chake na kulivuliwa nguo pamoja na kufunikwa macho na kutiwa pingu kama sehemu ya vitisho vya kisaikolojia.

Walidhani wangeuwawa wakati walipolazimishwa kusimama ukutani huku walinzi wa Iran wakiandaa bunduki zao. Waliambiwa ikiwa hawangekubali kukiri waliingia katika eneo la Iran, wangekabiliwa na kifungo cha miaka saba gerezani.

Iran imeueleza mkutano wa wanamaji hao na waandishi wa habari kuwa propaganda.

Wanamaji wote 15 waliozuiliwa na Iran kwa siku 13 walianza likizo ya wiki mbili na jamii zao kuanzia jana.