1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ligi ya mabingwa barani Ulaya kutimua vumbi viwanjani leo

7 Desemba 2010

Schalke 04 kuvaana na Benfica Lisabon huku timu zilizosalia zikipania kujishindania nafasi ya kusonga mbele katika kuelekea fainali ya kombe la mabingwa barani Ulaya

https://p.dw.com/p/QRp9
Kipa wa Schalke 04 Manuel Neuer atakuwa na kibarua cha kuzuia mikwaju ya washambuliaji wa Benfica LisbonPicha: AP

Tikiti saba zimeshanyakuliwa kuweza kuingia katika duru ya kabla ya robo fainali ya kombe la vilabu bingwa kuanzia kundi A hadi D, lakini Tottenham na Inter Milan katika kundi A, Schalke 04 na Lyon katika kundi B na Manchester United na Valencia katika kundi C zinapigania kila moja hii leo kunyakua usukani wa kundi lake, mnamo siku ya sita ya michuano hiyo ya ligi ya mabingwa barani Ulaya.

Kundi A linalozileta pamoja Twente ya Uholanzi, Tottenahm Spur ya Uingereza, Werder Bremen ya Ujerumani na Inter MiIlan ya Italy. Tottenahm na Inter Milan zimeshanyakua tikiti ya kuingia duru ijayo. Lakini waingereza na wataliana wanapimana nguvu nani anastahiki kunyakua usukani wa kundi lao. Tottenham Hotspurs wanaonyesha kuwa na nafasi nzuri, pindi wakitoka sare pamoja na Inter Milan wao ndio watakaoongoza kutokana na wingi wa magoli.

FC Twente ya Uholanzi imeshapata tikiti ya kusonga mbele baada ya Werder Bremen kupigwa kumbo.

Katika Kundi B Lyon ya Ufaransa itachuana na Hapoel Telaviv na Benefica Lisbon itapimana nguvu na Schalke 04 ya Ujerumani. Lyon na Schalke zimeshanyakuwa tikiti zao, lakini na hapo pia kinyang'anyiro kinahusu nani wa kuongoza kundi hilo. Ushindi wa Lyon hautasaidia kitu ikiwa Schalke 04 nayo pia itashinda. Pindi timu zote hizo mbili zikishindwa-hapo zitakuwa na pointi sawa. Na hapo Schalke ndio itakayoongoza kundi B.

Katika Kundi C Pambano kati ya Manchester United na Valencia ndilo litakaloamua nani watadhibiti usukani. Pindi waengereza wakishinda,usukani utakuwa wao.Itafaa kusema hapa kwamba Manchester United wana pointi 13 dhidi ya 10 za Valencia. Kundi hilo linazijumuisha pia Glasgow Rangers na Bursaspor ya Uturuki inayoburura mkia.

Katika Kundi D FC Barcelona imeshanyakua tikiti ya kuingia duru ijayo na pia inaongoza kwa pointi 11 katika kundi hilo linalozijumuisha pia Rubin Kazan ya Urusi, Copenhagen ya Danemark na Panathinaikos Athens ya Ugiriki. Tikiti ya pili itawania kati ya Copenhagen na Rubin Kazan. Rubin inakwenda nyumbani kwa Barcelona katika wakati ambapo Copenhagen inawakaribisha Panathinaikos ambao tokea hapo mguu mmoja uko nje.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Afp/Reuters

Mpitiaji:Abdul-rahman,Mohammed