1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Leipzig yatoka sare na Schalke

Bruce Amani
24 Aprili 2017

RB Leipzig walipoteza nafasi nzuri ya kupunguza pengo baina yao na vinara Bayern Munich kileleni mwa ligi hapo jana, wakati walikabwa kwa sare ya moja kwa moja dhidi ya Schalke.

https://p.dw.com/p/2bomv
Bundesliga FC Schalke 04 v RB Leipzig
Picha: Getty Images/Bongarts/L. Baron

Sare hiyo imeiwekwa Leipzig mbele ya nambari tatu Borussia Dortmund na pengo la pointi sita na Schalke wako katika nafasi ya 11 huku ikisalia mechi nne msimu kukamilika. Awali, Freiburg iliendeleza ndoto yake ya kucheza kandanda la Ulaya msimu ujao baada ya kupata ushindi wa kushangaza wa 2-1 dhidi ya Bayer Leverkusen hapo jana. Matokeo hayo yanaiweka Freiburg, mabingwa wa ligi ya divisheni ya pili msimu uliopita, katika nafasi ya sita, ambayo ina tiketi ya kucheza Europa League msimu ujao.

Yalikuwa matokeo mengine mabaya kwa Leverkusen, ambao walicheza katika hatua ya 16 za mwisho ya Champions League msimu huu, lakini wameshinda moja tu kati ya mechi zao 10 za mwisho na wako katika nafasi ya 12, pointi nne tu kutoka nafasi ya timu tatu za mkia. Siku ya Jumamosi, sare ya Bayern ya 2-2 dhidi ya Mainz, ambao pia walibanduliwa nje ya robo fainali ya Champions League na Real Madrid, ina maana miamba hao hawajashinda mechi zao nne za mwisho. Mats Hummels ni beki wa Bayern

Fußball Bundesliga Borussia Mönchengladbach v Borussia Dortmund Aubameyang  Ausgleich zum 2:2
Aubameyang anaongoza orodha ya ufungaji magoliPicha: Getty Images/AFP/P. Stollarz

Pierre-Emerick Aubameyang, mfungaji wa mabao mengi kwenye ligi kwa sasa, alifunga lake la 27 kwenye ligi, na kuisiadia Borussia Dortmund kupata ushindi wa 3-2 dhidi ya Borussia Moenchengladbach na kusonga hadi nafasi ya tatu. Mgabon huyo ana bao moja zaidi ya Robert Lewandowski wa Bayern Munich.

DFB Pokal

Wakati huo huo, Borussia Dortmund inataraji kuwaongezea Bayern Munich matatizo zaidi wakati timu hizo mbili zitashuka dimbani Jumatano wiki hii katika mchuano mkali wa nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la Ujerumani maarufuku kama DFB Pokal na kuizamisha ndoto ya Carlo Ancelotti kutwaa mataji mawili ya nyumbani katika msimu wake wa kwanza

Bayern na Dortmund zitakutana uwanjani Allianz Arena kutafuta tikiti ya kucheza fainali ya Mei 27 mjini Berlin. Kabla ya mechi hiyo, hapo kesho Borussia Moenchengladbach itawaalika Eintracht Frankfurt huku timu zote mbili zikilenga kutinga fainali kwa mara yao ya kwanza katika zaidi ya mwongo mmoja.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/Reuters
Mhariri: Iddi Ssessanga