1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kundi la pande nne kwa amani ya Mashariki ya Kati lashutumiwa

Mohamed Dahman28 Septemba 2008

Repoti mpya ya mashirika ya kimataifa ya misaada imelishambulia kundi la pande nne linaloshughulikia kuharakisha mchakato wa amani Mashariki ya Kati kwa kushindwa kutimiza malengo yake ya amani ya Israel na Wapalestina.

https://p.dw.com/p/FQLL
Jengo lilioko Rafah kusini mwa Ukanda wa Gaza.Picha: AP

Repoti hiyo inayosema kwamba kundi hilo la pande nne la kimataifa linashindwa kupiga hatua katika kuboregha maisha ya Wapalestina halikadhalika katika kuboresha matumaini ya kufikiwa kwa amani.

Repoti hiyo iliopewa jina Kundi la Pande Nne Mashariki ya Kati : Repoti ya Maendeleo inasema kwamba hakuna sifa yoyote iliowekwa na kundi hilo lenyewe ilioshuhudia maendeleo yoyote yale ya maana na hata baadhi ya malengo yake yamerudi nyuma.Katika malengo yote yaliorodheshwa na repoti hiyo ambayo yanazingatia taarifa za hivi karibuni za kundi hilo la pande nne takriban mengi yamepewa alama ya kushindwa na machache yamepewa hadhi ya mafanikio ya kiasi.

Repoti hiyo ilioandaliwa na muungano wa mashirika 21 ya misaada yakiwemo shirika la kimataifa la Oxfam,Save the Children ya Uingereza,World Vision Jerusalem na Care International la Uingereza inasema kwamba mwaka 2008 ulikuwa umeonekana na wahusika wote kuwa ni mwaka muhimu kwa mchakato wa amani.

Lengo la mkutano wa Annapolis mwezi wa Novemba ulioandaliwa na utawala wa Rais George W. Bush wa Marekani ulikuwa ni kufanikisha angalau sura ya makubaliano ambao utakuwa ni waraka utakaoweka ufafanuzi kwa ajili ya makubaliano ya mwisho ya amani bila ya kuwa lazima kwa kanuni zake kutekelezwa mwishoni mwa mwaka huu.

Kundi la Pande Nne linaloundwa na Umoja wa Ulaya, Umoja wa Mataifa,Urusi na Marekani lilianzisha jaribio kubwa katika mkutano wa Annapolis ulioandaliwa na utawala wa Rais George W. Bush wa Marekani mwezi wa Novemba kuhakikisha kwamba majukumu yalioko kwenye mpango wa ramani ya amani uliotangazwa na Bush kwa mara ya kwanza hapo mwaka 2002 na sheria ya kimataifa yanatekelezwa na pande zote mbili za mzozo.

Lakini kumalizika kwa mwaka wa 2008 kunakuja kwa haraka inaonekana muda uliopendekezwa na mkutano wa Annapolis utaishia kama vile wa mpango wa ramani ya amani Mashariki ya Kati bila ya kufikiwa kwa maendeleo ya maana juu ya masuala yoyote yale makuu.

Masuaa mengi ambayo kundi hilo pande nne limejipangia kuyafanyia kazi yalihusu kuboresha maisha ya Wapalestina pamoja na kuhakikisha kwamba Israel inachukuwa hatua ya kukomesha vitendo vinojenga uhasimu miongoni mwa Wapalestina.

Malengo yao yanazingatia taarifa ya Kundi hilo la Pande nne iliyotolewa Berlin tarehe 23 Juni na inajumuisha makaazi ya walowezi wa Kiyahudi,uwezo wa kupata huduma na nyendo za Wapalestina,matatizo ya kutatuwa mzozo Gaza mageuzi ya usalama ya Wapalestina,ahadi za wafadhili ambazo zitaendeleza kiuchumi maeneo yenye maendeleo duni ya Wapalestina yanayokaliwa kwa mabavu na Israel na hatimae maeneo hayo kuja kuendelzwa na sekta binafsi.

Repoti hiyo inalenga juu ya pengo kati ya maneno ya kundi hilo la pande nne na kushindwa kwake kuleta mabadiliko katika maeneo hayo.

Lugha kali katika mapendekezo ya repoti hiyo inatowa wito wa kuwepo kwa azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambalo litashughulikia taathira ya utanuzi wa makaazi ya walowezi wa Kiyahudi kwa jamii za Wapalestina na mchakato wa amani kwa mapana yake.

Katika kushughulikia suala la Gaza repoti inataka kufikia usuluhishi wa kukomesha uhasimu wa umwagaji damu kwa njia ya mazungumzo,kukomesha vikwazo vya Israel na hatimae kufufuwa shughuli zote za miradi ya kibinaadamu na maendeleo.

Repoti hiyo inatowa sura muhimu kwa mchakato wa amani kwa sababu makundi ya misaada mara nyingi yakiwa yenyewe yako katika maeneo husika au yakiwa na mtandao wa mawasiliano hapo yanakuwa yako kwenye nafasi imara zaidi kuweza kutathmini hatua za maendeleo.