1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kinyanganyiro cha Kombe la Ulaya 2008

Ramadhan Ali21 Novemba 2007

Uingereza,Ureno,Sweden na hata Uturuki zaweza kunyakua tiketi zao za Kombe la Ulaya jumatano hii:

https://p.dw.com/p/CPZu
Picha: AP

Leo jumatano tiketi 4 za mwisho za kombe lijalo la Ulaya –Euro 2008-nchini Uswisi na Austria zinagaiwa:Itakuwa maajabu iwapo Uingereza ,Ureno,Sweden na Uturuki,zitatateleza leo.

Kwa timu za kanda ya Amerika kusini,wao waania nafasi za kombe lijalo la dunia 2010 nchini Afrika Kusini-la kwanza barani Afrika:Colombia inaikaribisha Argentina inayoongoza kanda hiyo.Venezuela inaumana na Bolivia.

Ujerumani imeshakata tiketi yake ya kombe la Ulaya na mpambano wake wa leo na Wales, ni ada tuMacho yote ya mashabiki wao yatalengwa tena kwa Lukas Podolski.Jumamosi,Ujerumani iliikomea Cyprus mabao 4:0 na Podolski alikua ufunguo wa ushindi huo. Pigo pekee Ujerumani ililolipata katika safari yake ya Uswisi na Austria, lilitoka Jamhuri ya Czech.Ujerumani ilizabwa mabao 3:1.

Uingereza inakodolewa leo macho baada ya kuokolewa na Israel ilioilaza Russia jumamosi 2:1.England itahitaji alao pointi 1 kutoka Croatia uwanjani Wembley.Croatia inaongoza kundi hili.Ama Uingereza itaparamia leo kileleni mwa kundi hili au itapigwa kumbo kabisa nje ya mashindano.Suluhu itawaakoa.

Timu nyengine zinazotazamiwa kuifuata Uingereza katika finali za kombe hili ni Ureno,Sweden na Uturuki.Ureno,makamo-bingwa wa kombe lililopita 2004,inahitaji pia pointi 1 kutoka Finland.Na kwavile,inacheza nyumbani ina nafuu ya kuinyakua.Ikiwa ureno itateleza, ushindi mara 2 utaipatia Serbia Tiketi ya Uswisi.

Sweden halkadhalika, inahitaji alao sare ili kucheza finali ya kombe la Ulaya.Mahasimu wao leo ni Latvia. Wakiteleza nao hawatashiriki kombe la Ulaya tu, ikiwa Ireland ya kaskazini itatamba mbele ya Spain,iliokwishatia mfukoni tiketi yake.

Waturuki lazima watambe mbele ya Bosnia ikiwa wawapiku mahasimu wao Norway.Lakini wabosnia waliwaadhibu waturuki hapo Juni kwao Istanbul.Norway inaitembelea Malta.

Holland inacheza na Beloruss lakini, bila ya Van Niestelrooy na Seedorf.Hata kipa wa Manchester united Van der Sar,ameumia.

Mabingwa wa dunia-Itali wameshakata tiketi yao mwishoni mwa wiki ilipoitoa Scotland dakika za mwisho.Makamo-bingwa Ufaransa, wanaanza maandalio yao ya Kombe la Ulaya 2008 mjini Kiev,wakiwa na miadi huko na Ukrain.

Timu za kanda ya Amerika Kusini pia zinarudi leo uwanjani:Argentina inayoongoza kanda hiyo ina miadi na Columbia wakati Venezuela imeialika Bolivia.Argentina ndio timu pekee ambayo hadi sasa haikushindwa.Brazil ilimudu sare tu bao 1:1 jumapili iliopita na Peru.

Baadhi ya timu za taifa za Afrika zinateremka pia uwanjani jioni ya leo:

Afrika Kusini ina miadi nyumbani na Kanada.Uswisi,mwenyeji wa kombe la Ulaya inachuana na Nigeria iliotangaza jana kwamba itapiga kambi yake kwa kombe lijalo la Afrika la mataifa huko Malaga,Spain kuanzia Januari 4 mwakani.Algeria inaikaribisha nyumbani Mali wakati Angola inapanga kutamba leo mjini Paris mbele ya Guinea.