1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kesi ya maangamizi Cambodia.

Abdu Said Mtullya17 Februari 2009

Kesi ya mauaji halaiki imeanza kusikilizwa leo mjini Phnom Pehn , miaka 30 baada ya kuangushwa utawala wa Khmer Rouge nchini Cambodia.

https://p.dw.com/p/GvvM
Waliokuwa viongozi wa utawala wa Khmer Rouge wafikishwa mahakamani kujibu mashtaka juu ya maangamizi.Picha: AP

Kesi ya aliekuwa kiongozi wa utawala wa Khmer nchini Cambodia Kaing Guek Eav imeanza leo mjini Phnom Pehn.

Mtu huyo anakabiliwa na tuhuma za kuongoza mauaji halaiki na mateso ya watu wasiopungua alfu 15 katika jela moja.

Kesi hiyo iliyosubiriwa kwa muda mrefu, inasikilizwa kwenye mahakama inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa.

Mtuhumiwa, Kaing Guek Eav aliekuwa mwalimu wa hesabu alikuwa mkuu wa jela iliyokuwa inafahamika kwa unyama, ambapo watu hao alfu15 waliuliwa na kuteswa.

Kaing Guek Eav ambae pia anaitwa Duch anakabiliwa na mashtaka ya kuongoza jela hiyo kwa niaba ya utawala wa kikomunisti wa Cambodia mnamo miaka ya 70 .


Miaka 30 baada ya utawala wa wakomunisti kuangushwa, wawakilishi watano wa utawala huo leo wamefikishwa mbele ya mahakama maalum kujibu tuhuma za unyama uliotendwa na utawala wao mnamo miaka ya 70.

Waliongamizwa walikuwa pamoja na wasomi, watu ambao hawakuwa na nafasi katika utawala wa kikomunisti na maalfu ya watu wengine wa kawaida.Wote waliangamizwa katika sehemu zinazoitwa viwanja vya mauaji.Watu milioni 2 waliuliwa na utawala wa wakomunisti kwa kunyongwa au kutumikishwa kazi za harubu.


Watuhumiwa watano wamefikishwa mbele ya mahakama maalumu wakikabiliwa na mashtaka juu ya maamgamizi hayo.


Kwa watu wa Cambodia mahakama iliyoanzishwa mnamo mwaka 2006 baada ya mazungumzo ya karibu miaka 10 na Umoja wa Mataifa ni fursa ya mwisho ya kuweza kuwahukumu viongozi wa utawala wa wakoministi wa miaka ya 70.

Mshtakiwa mkuu Kaing Guek Eav alikamatwa mnamo mwaka 1999 baada ya mwandishi habari kumgundua akifanya kazi za kutoa misaada misituni.