1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kashfa ya ulimwengu wa dimba

5 Februari 2013

Hadaa katika viwanja vya dimba dunani ndio mada iliyohanikiza magazetini.Hata hivyo nafasi ya wahamiaji katika soko la ajira nchini Ujerumani,na jinsi sera ya familia inavyokosolewa,nazo pia zimezingatiwa

https://p.dw.com/p/17YDu
Kabumbu na fedhaPicha: Fotolia

Tuanzie na kuimarika nafasi ya wahamiaji kupata kazi nchini Ujerumani.Gazeti la "Lausitzer Rundschau" linaandika:

"Si muda mrefu ,sheria za Ujerumani kuhusu wageni zulikuwa zikiangaliwa kuwa ni kali.Hali imeanza kubadilika hivi sasa.Wasomi hawakutani tena na vizingiti wanapotafuta kazi.Kwa wale waliojipatia mafunzo ya kawaida ya kazi bado mambo si mazuri sana.Kunahitajika marekebisho.Na hasa ilivyokuwa kijerumani si lugha rahisi, mipango ya mapokezi ndiyo itakayomfanya mhamiaji aliyesoma aamue kusalia au la humu nchini.Kanuni za kiliberali kuwahusu wahamiaji ni sharti muhimu upande huo.

Mashabiki waduwaa

Fußball und Geld
Fedha na kabumbuPicha: Fotolia

Kashfa katika viwanja vya dimba imeushangaza ulimwengu wa michezo na mashabiki wa kabumbu nchini Ujerumani na ulimwenguni kwa jumla.Gazeti la "Landeszeitung" la mjini Lüneburg linahisi "hakuna ajuaye kama kweli hii ni kashfa kubwa kabisa kuwahi kutokea katika historia ya michezo kama shirika la Europol linavyosema.Sehemu ndogo tu ya visa vya udanganyifu ndiyo inayojulikana hadi sasa.Hata hivyo kila pambano la soka,lililofanyika kwa hadaa-naliwe dogo vipi,ni fedheha.Laghai katika kitu kinachopendwa zaidi ulimwenguni,ni sawa na kumzuzuwa mtoto mdogo anaelisakata dimba na kumvunja nguvu yeyote yule anaewashangiria vijana wadogo katika timu yake.Wao ndio daima wanaouangalia ulimwengu wa dimba kama unavyopigiwa upatu na vyombo vya habari kuwa ni mfano wa kuigwa.Bila ya kuwataja mashabiki wengineo wasiokuwa na idadi kote ulimwenguni.

Ruzuku kwa familia

Bundesfamilienministerin Schroeder legt Zehn-Punkte-Programm zur Beschleunigung des Kita-Ausbaus vor
Waziri wa familia wa serikali kuu ya Ujerumani Kristina SchröderPicha: dapd

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wamemulika pia uchunguzi uliofanywa na tume maalum iliyoundwa na wizara ya familia kutathmini marupu rupu yanayotolewa kwaajili ya familia.Tume hiyo ya wataalam imekosoa marupu rupu hayo na kusema yanawanufaisha zaidi wenye mapato ya juu.Gazeti la "Rhein Zeitung" linaandika:"Watoto,malipo ya wazee na kadhalika,hizo si rizuku.Marupu rupu hayo yameanza kutolewa ili kuifanya familia iweze kuishi kwa njia zinazostahiki nchini Ujerumani.Yanaweza kuangaliwa kama njia ya kuchochea lakini sio sababu ya watu kuamua kupata watoto.Kuanzisha mpango wa kufutilia mbali marupu rupu hayo kwasababu idadi ya watoto wanaozaliwa haikuongezeka,litakuwa kosa, sawa na kuendeleza utaratibu ulioko kwasababu ni chanzo cha mivutano.Ili kumaliza malumbano panahitajika mijadala ya kina.Tutaraji kwamba tume ya wataalam itabuni muongozo wa majadiliano hayo."

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Inlandspresse

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman