1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

kambi za mazoezi za timu za riadha kutoka Afrika.

Sekione Kitojo13 Agosti 2009

Jumamosi wiki hii inaanza rasmi michezo ya riadha ya ubingwa wa dunia mjini Berlin.

https://p.dw.com/p/J9Br
Mwanariadha wa China Liu Xiang akitimua mbio katika mashindano ya riadha ya dunia ya mita 110 wanaume kuruka viunzi mwaka 2007 mjini Osaka Japan.Picha: AP

Jumamosi wiki hii inaanza rasmi michezo ya riadha ya ubingwa wa dunia mjini Berlin. Katika miji mbali mbali ya Ujerumani tayari wako wanariadha maarufu kutoka kila pembe ya dunia. Si kila shirikisho la michezo linaweza kukodi maeneo ghali ya kufanyia mazowezi nchini Ujerumani. Wizara ya mambo ya kigeni imeyaalika mataifa 37 kutoka nchi masikini duniani kushiriki katika mashindano hayo , na kuwatayarishia kambi za mazowezi nchini Ujerumani. Philipp von Bremen ametembelea kambi za mazowezi za timu kutoka Botswana , Burkina Faso na Msumbiji.

Saa kumi jioni mazoezi yanaanza. Lakini katika uwanja mdogo wa michezo katika eneo la nyuma la ukumbi mkubwa wa michezo wa Esprit hakuna vitu vingi vinavyofanyika. Wanariadha wa Msumbiji na Burkina Faso wamepumzika tu katika wakati huu wa mchana, ambapo kuna hali ya joto kati kabisa katika majira haya ya mwaka. Robo saa baadaye anajitokeza Idrissa Sanou na mkufunzi wake Neya Alassane kutoka Hotelini , ambako si mbali sana na eneo hilo la uwanja wa michezo. Taratibu anaanza mkimbiaji huyo kutoka Burkina Faso kufanya mazoezi. Mwalimu wake anafurahishwa na hali ya utulivu inayopatikana katika eneo hili wanalofanyia mazowezi.

Hakuna magari mengi yanayopita hapa pamoja na treni. Kwa hali hii ya utulivu tunaweza kufanyakazi vizuri. Hii ni muhimu sana ili kuweza kufanya vizuri katika mashindano hayo ya dunia.

Mwanariadha huyo anayehudumiwa na Neya ndie pekee kutoka Burkina Faso, katika kambi hii ya mazoezi. Kwa wanariadha wote wawili kutoka Msumbiji hawana mwalimu waliefuatana nae. Mwanariadha anayekimbia mbio za mita 400, kuruka viunzi Kurt Couto anafanya mazoezi pamoja na Sanou kutoka Burkina Faso. Katika eneo la kivuli la uwanja huo anajenga sehemu ya kuanzia mbio.

Haieleweki iwapo wanariadha kutoka mataifa yanayoendelea wanaweza kujitayarisha katika mazingira kama haya kwa ajili ya mashindano makubwa ya dunia kama haya. Matayarisho ya wiki tatu nchini Ujerumani yanaweza kushindwa kutoa ufanisi unaotakiwa. Mwalimu Bobby Gaseitsewe pamoja na hayo anatoa shukrani nyingi, kwamba wizara ya mambo ya kigeni imeweza kuwapa maeneo hayo ya kufanyia mazowezi.

Hali hapa ni nzuri sana. Watayarishaji wameshughulikia kila kitu. Uwanja wa michezo ni mzuri, na hatuhitaji kusafiri mbali kwenda mazoezini, na pia tumepatiwa wataalamu wa viungo.

Hakuna mwanariadha aliyeko mjini Düsseldorf anatoa matumaini ya kupata medali. Sanou kutoka Burkina Faso atafurahi sana iwapo atafikia katika raundi ya pili. Kurt Couto kutoka Msumbiji anasema, anataka kufikia kiwango chake binafsi, na kama atafikia hadi katika nusu fainali , kwa kuwa kabla ya hapo katika msimu huu amekuwa ametupwa mbali. Na pia Bobby Gaseitsewe anaamini kuwa mkimbiaji wake kutoka Botswana anaweza kufanikiwa kupata medali.

Tuna timu ndogo sana. Tunaamini kuwa tutafanikiwa kufikia fainali, licha ya kuwa wanariadha wetu hawana kiwango cha kupata medali. Katika mbio za mita 400 tunamatumaini kwa wanariadha wanawake Amantle Montsho, Gable Garenamotse kuruka mbali , na pia Kabelo Kgosiemang kuruka juu.

Kama kuna mwanariadha mwenye nafasi ya kunyakua medali, ni Garenamotse. Ni pekee ambaye hufanya mazoezi pamoja na wenzake na siku za mapumziko hufanya mazoezi pekee. Mwanariadha huyo mwenye umri wa miaka 31 ni nyota wa timu nzima ya Botswana na alifikia fainali katika michezo ya mjini Peking.

Mwandishi Philipp von Bremen/ ZR/ Sekione Kitojo

Mhariri Mohamed Abdul-Rahman.