1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la Ujerumani laomboleza,na wakinamama washusha pumzi

Oummilkheir24 Mei 2007

Sauti zinapazwa kama wanajeshi wa Bundeswehr waendelee kulinda amani Afghanistan

https://p.dw.com/p/CHSs

Msiba kwa kuuliwa wanajeshi wa Ujerumani nchini Afghanistan na hukmu ya korti kuu ya katiba kuhusu gharama za ulezi wa watoto ndizo mada zilizotangulizwa mbele na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo.

Tuanze na msiba uliosababishwa na shambulio dhidi ya wanajeshi wa Ujerumani nchini Afghanistan.Maombolezi yameandaliwa jana katika uwanja wa ndege wa Köln/Bonn.Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wanachambua kama kuna haja au la ya kuendelea kuwepo wanajeshi wa Ujerumani nchini Afghanistan na pia jinsi Bundeswehr wanavyokabiliana na msiba huo.

Gazeti la KÖLNISCHEN RUNDSCHAU linahisi:

„Hata kama ilikua lazma na sawa kwa waziri wa ulinzi Franz Josef Jung ,kuwashukuru familia na jamaa za wahanga wa mashambulio hayo katika hotuba yake ya maombolezi,lakini,mahala maombolezi hayo yalikofanyika-ndani ya banda la ndege,hayalingani na tukio lenyewe.Si hayo tuu,lakini hata familia za wahanga wanalalamika dhidi ya usumbufu walioupata walipotaka kujua zaidi kuhusu kifo cha watoto na waume zao,au kuhusu wanajeshi waliojeruhiwa wanaohisi hakuna anaewashughulikia-yote hayo yanaonyesha jeshi la shirikisho Bundeswehr linahitaji kujirekebisha kuweza kukabiliana na mitihani ya opereshini kama hizi pakiwepo vifo,majeruhi na wengine waliochanganyikiwa.

Gazeti la THÜRINGER ALLGEMEINE la mjini Erfurt linauchambua mjadala huu ulioripuka upya wa kutumwa wanajeshi wa Ujerumani nchini Afghanistan kama ifuatavyo:

„Watu wanataraji wanasiasa wangekua na kipeo cha kuona mbali.Wahka huu wa ghafla katika mjadala kuhusu Afghanistan hauwezi kumtuliza yoyote.Muda mrefu hata kabla ya shambulio la hivi karibuni dhidi ya wanajeshi wa Ujerumani,wataalam wa masuala ya usalama walitoa mwito kudai mkakati wa aina mpya .Lakini madai yao hayakusikilizwa.Inavunja moyo unapoona maendeleo haba yaliyofikiwa tangu utawala wa wataliban ulipong’olewa madarakani mwaka 2001.”

Mada nyengine iliyoshughulikiwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo ni kuhusu uamuzi wa korti kuu ya katiba kuhusu gharama za ulezi wa watoto.Mama anaemlea peke yake mtoto aliyempata nje ya ndowa,alikua hadi sasa akipatiwa fedha za kumhudumia mwanawe kwa muda wa miaka mitatu tuu.Badala yake mama aliyeachwa akilipwa kwa muda wa miaka minane kwaajili hiyo hiyo.Hali hiyo ya kutokuwepo usawa,”ni kinyume na katiba” wanasema mahakimu wa korti kuu ya katiba.Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wanaiangalia hukumu hiyo kua ni pigo kwa vyama ndugu vya CDU/CSU. Gazeti linalochapishwa mjini Düsseldorf-HANDELSBLATT linaandika:

“Unafik umefikia mwisho wake.Korti kuu ya katiba imeamua mnamo dakika ya mwisho,katika kadhia ya sheria ya huduma za ulezi dhidi ya msimamo wa vyama ndugu vya CDU/CSU -machungu ambayo kamwe hawatayasahau.Korti kuu ya mjini Karlsruhe imetamka kinaga ubaga:Ikiwa mshahara wa mama unatosha kumshughulikia mtoto –hali hiyo haihitaji kuingizwa katika cheti cha ndowa.Vyama ndugu vya CDU/CSU,vimetia njiani sheria mpya ya kuwahudumia watoto inayowadhulumu mama waliozaa bila ya kuolewa .Uamuzi huo wa CDU/CSU uliwashangaza wengi na ulikua kinyume cha maagizo ya wataalam wao wa masuala ya kisheria.