1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jeshi la AMISOM laongezewa muda Somalia

1 Novemba 2012

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeupa ujumbe wa jeshi la Afrika la kulinda amani nchini Somalia AMISOM wiki moja zaidi kuendelea kuwa nchini humo wakati likijadili vikwazo vilivyopo vya silaha kwa taifa hilo.

https://p.dw.com/p/16ao3
NUR ZUR REDAKTIONELLEN NUTZUNG! A handout picture provided by the African Union-United Nations Information Support Team shows a Ugandan soldier serving with the African Union Mission in Somalia (AMISOM) standing at the back of an amoured fighting vehicle near a defensive position along the front-line in the Yaaqshiid District of northern Mogadishu, Somalia, 05 December 2011. In the face of a surge of car bombings and improvised explosive device (IED) attacks, the 9,700-strong African Union force continues to conduct security and counter-IED operations in and around the Somali capital. EPA/STUART PRICE / AU-UN IST PHOTO / HANDOUT HANDOUT EDITORIAL USE ONLY/NO SALES +++(c) dpa - Bildfunk+++ dpa 28561906
AU Soldat in ModagischuPicha: picture-alliance/dpa

Kurefushiwa muda kikosi cha AMISOM kunajiri wakati Baraza hilo lenye nchi wanachama 15 likijadili kuhusu ombi la Umoja wa Afrika la kutathmini kuhusu vikwazo vya silaha vilivyodumu miongo miwili dhidi ya nchi hiyo, ili kuisaidia serikali kupambana na wanamgambo wa kiislamu wenye msimamo mkali.

Wajumbe wa Umoja wa Mataifa walisema kuwa Baraza hilo bado limegawanyika kuhusu ombi la Umoja wa Afrika la kuanza kuruhusu uuzaji wa silaha kwa serikali ya Somalia. Pia limegawanyika kuhusu miito ya kuiruhusu Somalia kuuza nje makaa yaliyonaswa kutoka kwa wanamgambo wa al-Shabaab.

Jeshi la Uganda ni sehemu ya ujumbe wa AMISOM nchini Somalia
Jeshi la Uganda ni sehemu ya ujumbe wa AMISOM nchini SomaliaPicha: AP

Baraza hilo la Usalama lilipiga kura kwa kauli moja kurefusha muda wa kuhudumu jeshi la kulinda amani Somalia - AMISOM, ambao ulitarajiwa kumalizika Jumatano (31.10.2012), hadi tarehe saba mwezi huu wa Novemba. Wajumbe wa baraza hilo wamesema watatayarisha azimio ifikapo Jumatano wiki ijayo ambalo litawezesha kuongezwa muda huo hadi mwaka mmoja.

Mazungumzo kuhusu Somalia kumalizika

Aidha walisema wiki ijayo watamaliza mazungumzo ya faraghani kuhusu Somalia ambayo yalivurugwa na kimbunga Sandy, ambacho kilisababisha ukosefu wa umeme na uharibifu mkubwa mjini Manhattan na kusababisha mafuriko katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa kandoni mwa mto wa Mashariki ya jiji la New York.

Umoja wa Afrika umeliomba baraza hilo kutathmini upya vikwazo vya silaha dhidi ya Somalia ili kusaidia nchi hiyo kujenga upya jeshi lake na kuimarisha manufaa ya karibuni ya kijeshi dhidi ya kundi la al-Shabaab lenye mafungamano na mtandao wa kigaidi wa al-Qaeda.

Baraza hilo liliweka vikwazo hivyo mnamo mwaka wa 1992 ili kupunguza mtiririko wa silaha kwa wababe wa kivita, ambao mwaka mmoja baadaye walimuondoa madarakani kiongozi wa kiimla Mohamed Siad Bare na kuitumbukiza Somalia katika mgogoro wa vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Wanamgambo wa al-Shabaab walitimuliwa katika ngome yao ya mji wa bandari wa Kismayu
Wanamgambo wa al-Shabaab walitimuliwa katika ngome yao ya mji wa bandari wa KismayuPicha: AP

Wajumbe katika mkutano huo walisema Kenya pia inaunga mkono kutolewa kibali cha kuuza hifadhi hizo za makaa katika mji wa bandari wa Somalia, Kismayu, ambao wanajeshi wa Kenya chini ya mwamvuli wa AMISOM waliutwaa mwishoni mwa mwezi uliopita, licha ya Umoja wa Mataifa kupiga marufuku uuzaji wa makaa. Kuna mgawanyiko kuhusiana na suala hilo huku baadhi ya nchi zikihofia kuwa wafanyabiashara wa Kismayu wanaofanya ushawishi kwa ajili ya uuzaji wa makaa hayo huenda wakawa na uhusiano na al-Shabaab.

Baraza hilo huenda likakumbwa na ugumu kukubali mauzo ya makaa hayo kutoka Somalia kwa sasa. Wajumbe wamesema Marekani ni mojawapo ya nchi ambazo zinaweza kukubali kuuzwa makaa hayo kama serikali ya Somalia itaidhinisha. Lakini serikali hiyo bado haijaunga mkono suala hilo. Baraza la Usalama lilipiga marufuku uuzaji makaa kutoka Somalia mwezi Februari mwaka huu katika jaribio la kusitisha ufadhili wa kundi la al-Shabaab.

Mwandishi: Bruce Amani/Reuters

Mhariri: Josephat Charo