1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yazingira maeneo ya Jerusalem Mashariki

14 Oktoba 2015

Baraza la Mawaziri la Israel mapema leo, limepitisha hatua kadhaa za kupambana na ghasia zinazoendelea mjini Jerusalem.

https://p.dw.com/p/1Gnb4
Israel Jerusalem Sicherheitskräfte Gewalt Ausschreitungen
Vikosi vya usalama vya Israel mjini JerusalemPicha: Getty Images/AFP/A. Gharabli

Baraza hilo limeidhinisha polisi wa Israel kuzingira maeneo wanayoishi Waarabu Mashariki mwa Jerusalem, ama kuwazuia wasitoke majumbani mwao.

Taarifa iliyotolewa na Baraza hilo pia imesema imeidhinisha uvunjwaji wa makaazi ya Wapalestina waliowaita 'magaidi'.

Marekani kwa upande wake imelaani machafuko hayo, na kutoa wito wa kurejeshwa amani Jerusalem.

"Marekani inalaani vikali mashambulizi ya kigaidi dhidi ya raia wa Kiisrael. Na hadi sasa yamesababisha mauaji ya Waisrael watatu na kujeruhi wengine kadhaa, fujo zimekuwa zikiendelea kwa wiki kadhaa sasa. Machafuko haya na uchochezi mwengine wowote wa mashafuko lazima usite," alisema Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry.

Kerry amesema jana kwamba ana mpango wa kuelekea Mashariki ya Kati, kujaribu kutuliza fujo hizo baina ya Wapalestina na waisrael.

Machafuko Jerusalem

Jerusalem imeshuhudia umwagikaji mkubwa wa damu jana baada ya Wapalestina kufanya mashambulizi ya risasi ndani ya basi moja, pamoja na shambulizi lengine la gari iliyowagonga wapita njia kwa makusudi.

Katika shambulizi la basi, Mpalestina mmoja alifyatua risasi na mwengine alikuwa na kisu. Waisraeli wawili waliuawa na wengine 10 walijeruhiwa, kwa mujibu wa taarifa za madaktari pamoja na polisi.

Israel Anschlag in Jerusalem
Picha: Getty Images/I. Yefimovich

Wakati huo huo katika shambulizi la gari lilofanyika eneo la mji huo wanapoishi Wayahudi, Mpalestina mmoja akiwa ndani ya gari aliwavaa watu waliokuwa katika kituo cha basi na baadae alitoka na kisu na kumuua Muisrael mmoja na kuwajeruhi wengine wanane. Polisi wamesema mshambuliaji huyo aliuliwa kwa kupigwa risasi.

Chimbuko la machafuko

Machafuko haya yalianza Oktoba mosi, pale mtuhumiwa mmoja wa kundi la Hamas alipowaua kwa kuwapiga risasi walowezi wawili wa Kiyahudi mbele ya watoto wao, katika Ukingo wa Magharibi.

Mauaji hayo yalitokea baada ya fujo za mfululizo, zilizofanyika katika uwanja wa msikiti wa Al-Aqsa mwezi Septemba, baina ya vikosi vya Israel na vijana wa Kipalestina.

Awali machafuko hayo yalianzia Jerusalem ya mashariki pamoja na Ukingo wa Magharibi, na baadae kuenea hadi Gaza, ambapo vikosi vya Israel vimewaua Wapalestina tisa katika mapambano ya hivi karibuni.

Naye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amewatolewa wito Waisrael kufanya tathmini ya kina, kuchunguza iwapo vikosi vyake vya usalama vinatumia nguvu za kupindukia.

Mwandishi: Yusra Buwayhid/afpe/rtre

Mhariri: Grace Patricia Kabogo