1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yaendeleza mashambulio Ukanda wa Gaza

3 Machi 2008

-

https://p.dw.com/p/DGl2

GAZA

Rais Mahmoud Abbas wa Palestina ametangaza rasmi kusimamisha mawasiliano na Israel kupinga mashambulio ya angani yanayofanywa na taifa hilo la kiyahudi dhidi ya ukanda wa Gaza.Zaidi ya wapalestina 100 wameuwawa tangu Israel ilipoanzisha opresheni ya kijeshi jumatano iliyopita katika eneo hilo.

Mpatanishi wa upande wa wapalestina kwenye mazungumzo ya kutafuta amani Saeb Erekat amekosoa vikali hatua ya Israel na kuonya kwamba ikiwa mashambulio hayo yataendelea dhidi ya Ukanda wa Gaza basi ipo hatari ya kuzikwa kabisa kwa mazungumzo ya amani.

Shirika la kimataifa la haki za binadamu la Amnesty International,Umoja wa Ulaya na Umoja wa mataifa zimelaani mashambulio yanayofanywa na pande zote mbili waasi wa Kipalestina na wanajeshi wa Israel dhidi ya raia wasio na hatia katika Gaza.Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban- Ki Moon amezungumzia wasiwasi wake juu ya uwezekano wa kuenea kwa ghasia hizo na kusema anaunga mkono kwa dhati juhudi zote za kukomesha ghasia hizo na kuleta utulivu.

Aidha Katibu mkuu Ban Ki Moon katika kikao cha dharura cha baraza la usalama la Umoja wa mataifa alisema hatua ya Israel ya kulipiza kisasi mashambulio ya roketi ya wanamgambo wa kipalestina dhidi ya eneo la kusini mwa Israel imevuka mpaka.