1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ISLAMABAD : Musharraf ashinda uchaguzi tata wa rais

6 Oktoba 2007
https://p.dw.com/p/C7Hx

Tume ya uchaguzi nchini Pakistan imesema kwamba Rais Generali Pervez Musharraf anayetetea wadhifa wake ameshinda uchaguzi wa rais uliofanyika nchini humo leo hii.

Hata hivyo itabidi asubiri Mahkama Kuu kuthibitisha iwapo ugombea wake ulikuwa halali kabla ya kutangazwa rasmi kuwa mshindi.Kamishna mkuu wa uchaguzi Qazi Mohamed Farooq amesema kwamba Musharaff amejizolea kura 252 kati ya kura 257 zilizopigwa kwenye mabaraza mawili ya bunge la taifa.

Mahkama Kuu bado kuamuwa juu ya pingamizi za kisheria zilizowasilishwa na wapinzani wa Musharraf iwapo ugombea wake ulikuwa halali kutokana na kuendelea kushikilia wadhifa wa mkuu wa majeshi.Musharraf ameahidi kwamba iwapo atachaguliwa tena atan’gatuka wadhifa wa mkuu wa majeshi na kuapishwa kama kiongozi wa kiraia miaka minane baada ya kuchukuwa madaraka katika mapinduzi yasio na umwagaji damu.

Musharraf alikuwa amewekewa matumaini makubwa ya kushinda kipindi kengine cha miaka mitano madarakani baada wabunge 160 wa muungano wa upinzani kujiuzulu kupinga ugombea wake na chama cha waziri mkuu wa zamani Benazir Bhutto cha PPP kutoshiriki uchaguzi huo.