1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran, EU kutafuta msimamo wa pamoja makubaliano ya nyuklia

Sekione Kitojo
11 Januari 2018

Mataifa ya Umoja wa Ulaya na Iran yanatarajiwa kutafuta msimamo wa pamoja katika kuunga mkono makubaliano muhimu ya kinyuklia yaliyofikiwa mwaka 2015, katika mazungumzo mjini Brussels.

https://p.dw.com/p/2qfqu
Mohammad Javad Zarif Außenminister Iran
Picha: picture-alliance/dpa/A. Novoderezhkin

Umoja  wa  Ulaya, pamoja  na  mawaziri wa  mambo  ya  kigeni  wa Uingereza, Ujerumani na  Ufaransa watajiunga  pamoja  kutetea makubaliano  hayo  ya  kinyuklia  pamoja  na  Iran, ambayo yanadhibiti  azma  ya  Iran kujipatia  silaha  za  kinyuklia ili  kuweza nchi  hiyo  kupunguziwa  vikwazo  vikali  lakini  ambavyo Rais Donald Trump  wa  Marekani  amevikosoa  mara  kwa  mara  na  kutishia kujitoa  kutoka  katika  makubaliano  hayo.

USA UN-Generalversammlung Gabriel und Sarif
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani Sigmar Gabriel na waziri mwenzake wa Iran Mohammad Javad Zarif Picha: picture-alliance/dpa/B.von Jutrczenka

Wakati mkuu  wa  sera  za  mambo  ya  kigeni  wa  Umoja  wa Ulaya,  Federica Mogherini  anataka  kuliweka  suala  la  kinyuklia tofauti  na  masuala  mengine yenye utata  na  Iran, waziri  wa mambo  ya  kigeni  wa  Iran, Mohammad Javad Zarif pia atakabiliana  na  maswali  mazito  juu  ya  maandamano  ya  hivi karibuni  ya  kuipinga  serikali  ambayo  yamesababisha  watu 21 kuuwawa. Zarif  alisema  kwamba  nchi  yake inatekeleza  sehemu yake  ya  makubaliano  hayo.

"Kwa  bahati  mbaya  mjumbe  mwingine  wa  kamati  ya kuchukua  hatua  si tu  hajatimiza  majukumu  yake  lakini  pia anatekeleza  sera  za  uharibifu."

Makubaliano  ya  kinyuklia  na  Iran  yamejumuisha mzozo  mkubwa katika  Mashariki  ya  Kati na  ni  moja  kati  ya  mzizi  wa  masuala ambayo  dunia  haingependa  kuyaacha  yaongezeke. Amesema waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Ujerumani  sigmar Gabriel. Ameongeza  kwamba  kwa  mataifa  ya  Ulaya  kama  majirani  wa eneo  la  mashariki  ya  kati  hilo  ni  sehemu  kubwa  ya  usalama wa  mataifa  hayo.

Marekani yatafakari

Rais Donald Trump  wa  Marekani, ambaye  mwezi  Oktoba  alikataa kuthibitisha  kwamba  Iran  inatekeleza  makubaliano  yaliyofikiwa, lakini pia hakufikia kujitoa  kutoka  makubaliano  hayo, anatarajiwa  kuamua kesho  Ijumaa  iwapo atarefusha  hatua  ya  kuiondolea  Iran vikwazo vinavyohusiana  na  suala  hilo  la  kinyuklia.

US-Präsident Donald Trump
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: picture-alliance/abaca/O. Douliery

Umoja  wa  Ulaya   na  mataifa  mengine  yenye  nguvu  duniani umeonya  mara  kadhaa  kuwa  itakuwa  ni  makosa  kujiondoa kutoka  katika  makubaliano  hayo, yaliyofikiwa  pamoja  na  Iran kwa  muda  wa  miaka  2   kati  ya  Marekani, Uingereza, Ufaransa, China, Ujerumani  na  Urusi.

Waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Uingereza  Boris Johnson ameyaita  makubaliano  hayo, muhimu  ambayo  yanauweka ulimwengu  katika  hali  ya  usalama".

Brexit Boris Johnson
Waziri wa mambo ya kigeni wa Uingereza Boris JohnsonPicha: picture alliance/empics

"Ni muhimu  kwamba  tunaendelea  kufanya kazi  pamoja  na washirika  wetu  wa  mataifa  ya  Ulaya  kuendeleza makubaliano hayo  na  Iran, na usalama  na  ustawi  unaotokana  na makubaliano hayo unawafikia  watu  wa  Iran na  dunia  kwa  jumla.

Kwa  mujibu  wa  vyanzo  nchini  Marekani, Trump  hajafanya maamuzi  hadi  ilipofika  jana  Jumatano, wakati Johnson aliliambia bunge  la  Uingereza  siku  ya  Jumanne  kwamba, Uingereza inawataka  "marafiki  zao katika  Ikulu  ya  Marekani  ya  White House kutoyatupa  makubaliano  hayo".

Mwandishi: Sekione Kitojo /afpe

Mhariri: Grace Patricia Kabogo