1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hali katika jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo

Hamidou, Oumilkher11 Novemba 2008

Nkunda asema haamini kama wanajeshi wa Angola wanapigana upande wa serikali

https://p.dw.com/p/FrVn
Laurent Nkunda na walinzi wake huko TeberoPicha: AP


 Kiongozi wa waasi Laurent Nkunda amehakikisha,wataendelea kuheshimu uamuzi wa upande mmoja wa kuweka chini silaha kaatika eneo la mashariki la jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo.


Tangu jumapili mchana,hakuna mapigano makubwa yaliyoripotiwa.Jana vikosi vya pande zote mbili,waasi na wanajeshi wa serikali,walikua bado wametangana kwa mita mia kadhaa karibu na Goma-hayo lakini ni kwa mujibu wa Umoja wa mataifa unaojaribu bado kuwarejesha nyuma mahasimu hao.


Laurent Nkunda,aliyetishia kwa mara nyengine tena kuitimua serikali madarakani,anaamini,hali ya mambo inaweza kubadilika licha ya serikali ya mjini Kinshasa kukataa kuanzisha mazungumzo ya ana kwa ana pamoja na waasi.


„Watu wanabidi waitanabahishe serikali ya Kinshasa,na nna furahi sana kuona kwamba ulimwengu unaanza kuzungumzia umuhimu wa kupatikana ufumbuzi wa kisiasa“-amesema kiongozi huyo wa waasi.


Amekanusha hata uvumi eti mazungumzo ya kichini chini yanafanyika pamoja na serikali ya Kinshasa,na kuzisuta pia tuhuma za wafuasi wake mwenyewe wanaodai kwamba wanajeshi wa Angola wanapigana upande wa vikosi vya serikali.


Wakati huo huo wataalam wa shirika la kimataifa linaloshughulikia mizozo ulimwenguni-ICG,wamesema katika ripoti iliyochapishwa hivi karibuni na gazeti la Wall Street Journal,kwamba waasi wa Laurent Nkunda „wamepatiwa misaada ya kijeshi na madawa kutoka Rwanda.“


„Wanawaandikisha wapiganaji wao toka katika kambi za wakimbizi wa kitusti na toka vikosi vinavyozurura vya jeshi la Rwanda,hata kama jeshi la Rwanda halihusiki moja kwa moja ,kinyume na vile serikali ya Kinshasa inavyodai-ripoti hiyo imesema.


Jumuia ya maendeleo kusini mwa Afrika SADC,ambayo viongozi wake walikutana jumapili iliyopita mjini Johannesburg imeelezea utayarifu wa kutuma wanajeshi wa kulinda amani mashariki ya jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo.


Akihojiwa na kituo cha CNN kuhusu mkutano huo wa SADC waziri wa habari wa jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo, Lambert MENDE OMALANGA alisema


„Waziri mku wetu na mie binafsi tumetokea Goma.Tulikuwepo wiki nzima ili kujaribu kuwatanahabisha ,Nkunda na wanamgambo wake,waache kuuwa watu,waache kupora mali na waje wazungumze na serikali namna ya kuupatia ufumbuzi ncha moja ya mzozo huu ambayo ni ya kitaifa.Kwasababu kuna ncha ya kitaifa na ncha ya kimkoa-na rais wetu alikwenda Nairobi kuzungumza na rais Kagame.“


Umoja wa Ulaya umeelezea hofu kutokana na kuzidi kuharibika hali ya mambo kaatika jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo.Hata hivyo haufikirii kutuma wanajeshi nchini humo.


Mapigano ya miezi miwili katika eneo la Kivu kaskazini yamegharimu maisha ya watu wasiiopungua 100 na wengine zaidi ya laki mbili na nusu kuyapa kisogo maskani yao.


Shirika la kimataifa la msalaba mwekundu limesema limeanza upya kuwapatia chakula watu 65 elfu waliotawanyika katika zoni ya Kibati,umbali wa kilomita 12,kaskazini mwa Goma.




►◄