Gesi iliyopigwa maarufuku ilitumika kuwakandamiza waandamanaji katika nchi za kiarabu
21 Desemba 2011Akielezea jinsi gesi hiyo ya kutoa machozi ilivyomuathiri, mkuu mmoja wa masoko nchini Misri, Mahmoud Hassan, amesema alijisikia dhaifu na alipatwa na kizunguzungu mara tu baada ya kuvuta gesi hiyo.
Mahmoud ambaye alikimbizwa hospitalini mwezi uliopita, kufuatia maandamano ya kuupinga utawala jijini Cairo, ameshuhudia jinsi gesi hiyo ilivyoathiri raia wengi na anakumbuka jinsi mikono yake ilivyokuwa ikitetemeka bila kukoma.
Wanaharakati wa nchini Misri wamesema gesi iliyotumika kuwatawanya waandamanaji msimu huu, ilikuwa na nguvu mara dufu ukilinganisha na ile iliyotumiwa na vikosi vya serikali ya Hosni Mubarak, dhidi ya maandamano ya siku 18 yaliyouangusha utawala wa kiongozi huyo wa kiimla.
Sumu hiyo iliyoko katika gesi hiyo pia iliunguza ngozi na mapafu ya waandamanaji hao. Wachunguzi wa mambo wanahisi kuwa gesi hiyo ndiyo iliyosababisha vifo vya karibu raia wanane nchini Bahrain, tangu mwezi wa Februari mwaka huu.
Madaktari wa jijini Sanaa, Yemen wamesema waandamanaji waliopelekwa hospitalini wakati wa wimbi hilo, walikuwa wamepooza na wasiojitambua, na baada ya vipimo walionekana kuathiriwa na gesi ya machozi walioivuta.
Sumu hiyo ni poda iliyotengenezwa na kemikali ya ortho-chlorobenzylidene-malononitrile, maarufu kama CS. Kemikali hiyo ilitumika katika miaka ya hamsini, kudhibiti mikusanyiko ya watu na kutokana na ukali wake, ikatafutwa kemikali nyingine mbadala aina ya chloroacetophenone CN.
Makombora ya gesi za machozi yaliyokusanywa katika maeneo yaliyofanyika maandamano katika nchi za kiarabu yana nembo za makampuni mbalimbali. Idadi kubwa ya makombora yaliyookotwa katika viunga vya Tahrir, jijini Cairo, yana nembo za kampuni ya Marekani-Combined Tactical Systems (CTS) -inayotengeneza kemikali zinazowasha na vifaa vya kijeshi kwa ajili ya majeshi ya polisi na ulinzi sehemu mbalimbali duniani.
Kwa mujibu wa maelezo ya mwanaharakati wa Shirika la Haki za Binadamu la Misri, Sherif Azer, makombora mengine yaliyookotwa katika nchi hizo za Mashariki ya Kati yana nembo za Kampuni ya Federal Laboratories and British Weapons Manufacturer Chemring yenye makao yake makuu nchini Marekani.
Kwa upande mwingine, makombora yaliyookotwa nchini Bahrain kufuatia maandamano ya mwaka huu yana nembo ya Kampuni moja ya Marekani ijulikanayo kwa jina la NonLethal Technologies.
Na wakati makampuni ya Federal Laboratories, CTS, Chemring na Kampuni ya Ulinzi ya Ufaransa, SAE Alsetex, yakiwa katika orodha ya kusambaza silaha katika nchi za Kiarabu, CTS ni kampuni inayoongoza katika kupeleka askari wa kutuliza machafuko katika serikali ya Yemeni.
Wakati wanaharakati wa haki za binadamu wakishindwa kuthibitisha tuhuma hizo, wachunguzi wengine wa mambo wanahisi vikosi hivyo vya serikali katika nchi za kiarabu walitumia gesi za machozi zilizoisha muda wake, na hiyo ndiyo sababu athari zake kwa waandamanaji zilikuwa mbaya sana.
Gesi za kutoa machozi, aina ya CS zina uwezo wa kudumu kwa kati ya miaka mitatu mpaka mitano lakini wanaharakati wa jijini Manama, Bahrain na Misri wamesambaza picha za makombora yanayoonesha kutengenezwa zaidi ya miaka kumi iliyopita.
Wizara ya Afya nchini Misri imekanusha tuhuma hizo, na uchunguzi zaidi unaendelea.
Mwandishi: Pendo Paul Ndovie/IPS
Mhariri:Josephat Charo