1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mgogoro wa Georgia

Mtullya, Abdu Said13 Agosti 2008

Mpango wa amani juu ya kutatua mgogoro wa Georgia wawasilishwa.

https://p.dw.com/p/EwGm
Mgogoro wa GeorgiaPicha: AP

Urusi  na Georgia zimekubaliana na mpango  uliopendekezwa  na rais Nicolas Sarkozy  wa   Ufaransa juu ya kutatua mgogoro baina yao nchi   zao.

Lakini Urusi  imesema,lazima Georgia iyarudishe  majeshi  yake yote kambini.

Rais Nicolas Sarkozy  ambae  kwa sasa ni rais wa  Umoja wa Ulaya  amefikia mapatano na Urusi na  Georgia juu ya mpango wa  kutatua mgogoro wa   nchi hizo mbili  baada  ya vita vya  siku tano.

Kwa mujibu wa mpango huo, Urusi na Georgia zitarudisha majeshi yao mahala yalipokuwapo kabla  ya vita kuanza.

Mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya   wanajadili mpango huo mjini Brussels.

Hatahivyo Urusi imesema itaondoa majeshi yake    kwenye ardhi ya Georgia ikiwa Georgia itayarudisha  majashi yake kambini.

Waziri wa mambo ya nje  wa Urusi Sergei Lavrov amesema  hayo leo kwenye mkutano  na wandishi  habari mjini Moscow.

Ameeleza  kuwa  ikiwa majeshi ya Georgia yatarudishwa  kambini, Urusi pia itayarudisha  nyumbani majeshi yake yote kutoka Georgia.

Hatahivyo amesema kuwa walinda amani wa Urusi wataendelea kuwapo katika Ossetia ya kusini.

Katika hatua  nyingine yenye lengo la kutatua mgogoro baina ya  nchi yake na Urusi rais wa Georgia   Saakashvili amesema  sasa pana ulazima wa kupitishwa  azimio la baraza  la usalama la Umoja wa  Mataifa.

Baada ya  mazungumzo yake na rais Dmitri Medvedev wa Urusi rais Nicolas Sarkozy  alifahamisha mjini Moscow kuwa Urusi na Georgia zimekubaliana na mpango wa vipengee sita juu ya   kuanza mazungumzo ya kuutatua mgogoro wa Georgia.

Lakini waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Lawrov amesema  itakuwa vigumu kwa nchi yake  kufanya mazugumzo ya ana kwa ana na rais Saaka shvili.

Waziri huyo ameeleza kuwa rais huyo wa Georgia  ametenda  uhalifu dhidi ya watu wa Urusi bila ya  kuifikiria madhara yake, na lingekuwa jambo bora  iwapo angeliondoka.

Watu wapatao  mia moja alfu wanakadiriwa kuwa  wamepoteza makao yao kufuatia mapigano ya siku   tano baina ya majeshi ya Uruis na ya Georgia.

Hatahivyo Urusi jana  ilitangaza hatua ya kusimamisha  mapigano  baada ya kusema kuwa  ilifikia shabaha yake. Wakati huo huo Urusi imefahamisha kuwa  ilipoteza askari wake 74 katika mapambano  na Georgia. Askari wake wengine 171  walijeruhiwa na 19 hawajulikani walipo.