1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Georgia yaondowa vikosi Ossetia Kusini

Mohamed Dahman10 Agosti 2008

Georgia imeondowa vikosi vyake kutoka jimbo lililojitenga la Ossetia Kusini ambapo imekuwa ikipambana na vikosi vya Urusi kuwania udhibiti wa jimbo hilo.

https://p.dw.com/p/Etqa
Zana za kurushia maroketi za Georgia katika kijiji cha Georgia kilioko Ossetia Kusini.Picha: AP

Jeshi la Urusi hata hivyo linasema vilkosi vya Georgia bado viko katika jimbo hilo.

Tangazo la kuondolewa kwa vikosi vya Georgia linafuatia siku tatu za mapigano za harakati za Georgia kudhibiti jimbo hilo kutoka kwa wapiganaji wanaotaka kujitenga wanaoungwa mkono na Urusi na kupelekea Urusi kuingiza vikosi vyake Ossetia Kusini na kufanya mashambulizi ya anga ndani ya Georgia.

Georgia imeiomba Marekani iwe msuluhishi wa mzozo huo na Urusi juu ya jimbo hilo lililojitenga la Ossetia Kusini.

Rais George W. Bush wa Marekani ameitaka Urusi kukomesha mashambulizi ya mabomu dhidi ya Georgia

Bush amesema Marekani inashirikiana na washirika wao wa Ulaya kuanzisha usuluhishi wa kimataifa na makundi husika kuanza upya mazungumzo na kwamba Urusi inabidi iunge mkono juhudi hizo ili kwamba amani iweze kurudishwa haraka iwezekanavyo.

Vikosi vinavyotaka kujitenga vya Georgia vimekuwa vikukusanyika kwenye mpaka wa Georgia wa mkoa wa Zugdidi na televisheni ya NTV ya Urusi imeripoti kwamba vikosi zaidi vya Urusi vimetuwa huko Abkhazia vikielekea kwenye mpaka huo huo.

Urusi pia imetuma kikosi cha majini kuzinga mwambao wa Georgia wa Bahari Nyeusi.