GAZA : Hamas yasitisha suluhu na Israel
25 Aprili 2007Kitengo cha kijeshi cha Hamas kimetangaza kumalizika kwa usitishaji wa mapigano wa miezi mitano huko Gaza hapo jana kwa kuifyetulia maroketi Israel.
Kitengo hicho kimesema kimefyatuwa maroketi kutoka Ukanda wa Gaza kutokana na mauaji ya Wapalestina tisa mwishoni mwa juma yaliofanywa na vikosi vya Israel.Maroketi hayo yamesababisha uharibifu mdogo na hakuna majeruhi wakati taifa hilo la Kiyahudi likisheherekea siku ya uhuru wake.
Akizungumza mjini Rome Italia Rais Mahmoud Abbas wa Palestina amesema ukiukaji huo wa suluhu ni tukio lisilo la kawaida ambalo halitadumu na ameiomba Israel kuchukuwa hatua ya kujizuwiya ili jambo hili lisitokee tena.
Waziri wa Ulinzi wa Israel Amir Peretz ameionya serikali ya umoja wa kitaifa ya Palestina ilioundwa mwezi uliopita na kundi la Kiislam la Hamas na lile la Fatah la Rais Abbas dhidi ya kuruhusu mashambulizi zaidi ya maroketi kwa Israel.