1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

G8 wailaani Korea Kaskazini

Admin.WagnerD11 Aprili 2013

Mawaziri wa mambo ya kigeni wa mataifa manane yaliyoendelea zaidi kiviwanda wameungana kuilaani Korea Kaskazini, na kuitaka nchi hiyo kukomesha mara moja kutoa vitisho vya kivita

https://p.dw.com/p/18EPY
Mawaziri wa mambo ya nje wa mataifa ya G8 wakiwa jijini London.
Mawaziri wa mambo ya nje wa mataifa ya G8 wakiwa jijini London.Picha: Reuters

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Guido Wester Welle, amesema katika siku ya pili ya mkutano wa mawaziri hao unaoendelea jijini London, Uingereza, kuwa mataifa yote ya G8 yanaaminini kuwa kuongezeka kwa matamshi hayo ya kuchochea vita kutoka kwa Korea Kaskazini lazima kusitishwe.

Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Guido Westerwelle
Waziri wa mambo ya kigeni wa Ujerumani, Guido WesterwellePicha: DW/B.Riegert

"Suala la kwa nini matamshi hayo ya kuchochea vita yanaongezeka – ingawa ni muhimu, lakini halina uzito mkubwa. Muhimu zaidi ni kwamba matamshi hayo hayapelekei kuripuka kwa vita. Na ndio maana ni muhimu sasa kuona jumuiya ya kimataifa ikiwajibika na kuzungumza kwa sauti moja. Siyo pekee nchi za magharibi zinazobidi kuwa na msimamo mmoja, bali pia China na Urusi. Maoni yangu ni kwamba nchi hizi mbili pia zingependelea hivyo," alisema Wester Welle.

Korea kaskazini imetoa vitisho dhidi ya Korea Kusini, Japan na Marekani na inaonekana kujiandaa kufanya majaribio kadhaa ya makombora ambayo wadadisi wanasema huenda ikayafanya kwa wakati mmoja. Waziri wa mambo ya kigeni wa Uingereza, William Hague, alisema nchi iko njia panda hivi sasa, na inaweza kuishia kuwa taifa lililosambaratika na kutengwa, iwapo itashindwa kushiriki mazungumzo.

Tisho la mfululizo wa majabirio ya makombora

Jeshi la Korea Kusini limenukuliwa leo likisema kuwa Korea Kaskazini inaweza kufanya majaribio hayo ya makombora muda wowote, na kwamba mitambo ya kuvurumishia makombora hayo imekwishawekwa katika pwani ya mashariki ya nchi hiyo. Shirika la habari la Yonhap la mjini Seoul limesema kuwa mitambo karibu mitano imeonekana katika mkoa wa mashariki wa Hamkyung Kusini.

Shirika hilo likimnukuu afisa wa serikali ya Korea Kusini ambaye halikumtaja jina, limesema kuwa zipo dalili za wazi kuwa Korea Kaskazini inaweza kuvurumisha makombora aina ya Musudan, Scud na Nodong kwa wakati mmoja. Makombora ya Scud yana uwezo wa kwenda umbali wa kilomita kati ya 300 na 500, na Nodong yanaweza kwenda kati ya kilomita 1,300 hadi 1,500.

Mawaziri wa mambo ya kigeni wa mataifa yaliyoendelea zaidi kiviwanda G8 wakiwa katika mkutano wao mjini Londo Uingeraza Alhamisi 11.04.2013.
Mawaziri wa mambo ya kigeni wa mataifa yaliyoendelea zaidi kiviwanda G8 wakiwa katika mkutano wao mjini Londo Uingeraza Alhamisi 11.04.2013.Picha: Leon Neal/AFP/Getty Images

Wakati wasiwasi ukizidi kutanda katika rasi ya Korea, katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kujihami NATO, Anders Fogh Rasmussen, amewasili Korea Kusini kwa ajili ya mazungumzo, katika ziara ya kwanza kabisa ya kiongozi huyo wa jumuiya hiyo ya kijeshi.

Korea Kusini pia imeisihi Korea Kaskazini kufungua tena eneo la viwanda la Kaesong lililofungwa tangu siku ya Jumanne. Eneo hilo linaendeshwa kwa pamoja kati ya Korea mbili, na waziri wa muungano wa Kusini, Ryoo Kihl, ameitaka kaskzini irudi katika meza ya mazungumzo. Lakini afisa kutoka wizara hiyo alisema baadaye kuwa taarifa hiyo ya waziri Kihl Jae haikuwa pendekezo rasmi la kuanzisha tena mazungumzo.

Mwandishi: Iddi Ismail Ssessanga/dpae,
Mhariri: Jospehat Charo