1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gülen akosoa mfumo wa sheria wa Uturuki

5 Agosti 2016

Imam wa zamani wa Uturuki, Fethullah Gülen, anaetakiwa na Uturuki kwa tuhuma za kuandaa njama iliyoshindwa ya mapinduzi, ameukosoa mfumo wa sheria wa Uturuki akisema si huru na unadhibitiwa na utawala wa kimabavu.

https://p.dw.com/p/1Jc66
Fethullah Gulen
Picha: picture-alliance/dpa/Fgulen.Com

Amri ya kutaka akamatwe imam huyo wa zamani iliyotolewa jana na mahakama ya mjini Istanbul inamtuhumu Fethullah Gülen anaeishi uhamishoni Pennsylvania- Marekani tangu mwaka 1999,"kuandaa njama ya mapinduzi july 15 iliyopita-njama iliyoitikisa serikali kwa muda wa masaa kadhaa na kusababisha watu wasiopungua 272 kuuwawa.

Amri hiyo inawafungulia njia viongozi wa serikali ya mjini Washington kumrejesha nyumbani mpinzani huyo mkubwa wa rais Recep Erdogan.

"Amri ya kukamatwa haitobadilisha chochote kuhusu hadhi yangu wala msimamo wangu. Nimelaani mara kwa mara njama hiyo ya mapinduzi nchini Uturuki na nimekanusha kujua chochote au kuhusika kwa aina yoyote ile. Hakuna asiyejua kwamba mfumo wa sheria wa Uturuki si huru,kwa hivyo amri hii ya kukamatwa ni ushahidi mwengine unaoonyesha jinsi rais Erdogan anavyofuata mtindo wa utawala wa kimabavu na kuachilia mbali mfumo wa demokrasia".Anasema Gülen.

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani kuitembelea Uturuki

Rais Erdogan amesema jana usiku kwamba waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani John Kerry atafika ziarani nchini humo mwishoni mwa mwezi huu-hiyo ikiwa ziara ya kwanza kufanywa na mwanadiplomasia wa ngazi ya juu wa nchi za magharibi tangu njama iliyoshindwa ya mapinduzi,july 15 iliyopita. Lakini wizara ya mambo ya nchi za nje ya Marekani haijathibitisha bado tarehe hiyo.

Rais Recep Tayyip Erdogan wa Uturuki
Rais Recep Tayyip Erdogan wa UturukiPicha: Reuters

Madai ya Uturuki dhidi ya Gülen yanatishia kuutia sumu uhusiano kati ya Marekani na Uturuki. Marekani inaitaka serikali ya mjini Ankara itowe ushahidi timamu wa kuhusika imam huyo na njama hiyo ya mapinduzi. Serikali ya mjini Washington imesema kwa mara nyengine tena jana kwamba utaratibu huo unahitaji muda mrefu. Wizara ya sheria inatathmini ili kuhakikisha kama hati zilizowasilishwa zinatosha kumrejesha nyumbani mtuhumiwa-amesema hayo msemaji wa wizara ya mambo ya nchi za nje ya Marekani Mark Toner.

Katika kipindi cha wiki mbili zinazokuja ujumbe utakaoongozwa na mawaziri wa mambo ya nchi za anje bna wa sheria wa Uturuki watakwenda Marekani kuelezea jinsi Gülen alivyohusika na njama hiyo ya mapinduzi-amesema haso rais Erdogan jana usiku.

Kamata kamata inaendelea

Mpwa wa Fethullah Gülen,Muhammet Said Gülen ametiwa jela jana usiku baada ya kushikiliwa na polisi tangu julai 23 iliyopita.

Polisi wakipiga doria mjini Istanbul
Polisi wakipiga doria mjini IstanbulPicha: Getty Images/B. Kara

Msako dhidi ya wafuasi au mashabiki wa Gülen tangu wa kweli mpaka wa kubuni unaendelea nchini Uturuki. Kwa mujibu wa wizara ya mambo ya ndani watu karibu 26.000 wamekamatwa na 50 elfu wamefukuzwa kazi.

Mwandishi: Hamidou Oummilkheir/AFP

Mhariri: Yusuf Saumu