1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

FIFA yampata mfadhili mpya

19 Machi 2016

Rais wa FIFA Gianni Infatino amesema kuwa tayari kumeanza kuonekana dalili za mabadiliko katika shirikisho hilo la kandanda ambalo katika siku za hivi karibuni lilikuwa limegubikwa na kashfa za rushwa

https://p.dw.com/p/1IGBa
FIFA Präsident Gianni Infantino
Picha: Getty Images/AFP/G. Caddick

Infantino ametangaza hapo jana shirikisho hilo kuingia mkataba wa ufadhili na kampuni ya kichina ya Wanda Group.

Mkataba wa ufadhili huo ambao utadumu hadi mwaka 2030 na ukihusisha fainali nne zijazo za kombe la dunia umekuja siku moja baada ya shirikisho hilo lenye makao yake makuu nchini Uswisi kutangaza kupata hasara ya dola za kimarekani milioni 122 katika kipindi cha mwaka 2015 ambayo ni hasara yake ya mara ya kwanza tangu mwaka 2002.

Ufadhili huo utamsaidia Ifantino, ambaye alichaguliwa mwezi uliopita kuchukua mikoba ya aliyekuwa Rais wa shirikisho hilo Sepp Blatter kutimiza ahadi yake aliyoitoa kwa wanachama 209 wa shirikisho hilo wakati wa kipindi cha kampeni kuwania nafasi hiyo kuiwezesha FIFA kuwa na uwezo mkubwa wa kifedha.

FIFA ilitumbukia katika mgogoro mwaka jana ambapo uchunguzi dhidi ya viongozi kadhaa wa shirikisho hilo umekuwa ukiendelea nchini Marekani na pia Uswisi kuhusiana na kashifa mbalimbali zikiwemo za matumizi mabaya ya madaraka ndani ya shirikisho hilo zinazowakabili.

Mwanandishi: Isaac Gamba/Reuters
Mhariri: Bruce Amani