1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Fainali ya kombe la dunia la kandanda la wanawake leo

17 Julai 2011
https://p.dw.com/p/RaIg
Baadhi ya wachezaji wa Marekani (kushoto na wenzao wa Japan ( kulia) wakisherehekea wakati wa moja wapo ya mechi zao, kabla ya fainali ya leoPicha: AP/DW-Fotomontage

Mashindano ya kombe la kandanda la usiku baada ya pambano la fainali mjini Frankfurt kati ya Marekani na Japan.wanakandanda la dunia la wanawake, mjini Frankfurt Mashindano haya ambayo safari hii yamefanyika Ujerumani yalianza Juni 26. Marekani imeshalitwaa kombe hilo mara mbili 1991 na 1991, wakati Japan ikishiriki katika fainali kwa mara ya kwanza .

Historia inaonekana kuwa upande wa timu ya Marekani kwani haijawahi kushindwa na Wajapani katika jumla ya michuano 25 tangu 1986, ikiwa imeshinda mara 22 na kutoka sare mara tatu. Lakini kocha wa Japan, Norio Sasaki anasema,mambo yamebadilika na timu yake imejiimarisha zaidi, hasa baada ya kuwatoa wenyeji wa mashindano haya Ujerumani, katika mchezo wa robo fainali na kuiangusha Sweden katika pambano lao la nusu fainali

Nahodha wa Japan Homare Sawa mwenye umri wa miaka 32, ambaye ameshacheza katika mashindano matano ya kombe la dunia, amekataa kusema kama atafikiria kustaafu pindi watafanikiwa kuandika historia kwa kutawazwa mabingwa. Amesema, anachokizingatia wakati huu, ni pambano la leo na mustakbali wake ni suala la baadae

Kocha wa Marekani, Pia Sundhage kwa upande wake ana matumaini kuwa wataibuka na ushindi na kuweka historia ya kulinyakua kombe hilo kwa mara ya tatu. Ameungama hata hivyo kuwa anadhani itakua mechi ngumu, lakini watasaka njia za kuibuka na ushindi. Kikosi cha Marekani ni pamoja na wachezaji wake 14 waliokuwemo katika timu yao ya Olimpik 2008 ilionyakua medali ya dhahabu katika soka la wanawake.

Jana katika pambano la kutafuta mshindi wa tatu, Sweden iliibwaga Ufaransa mabao 3 -1 mjini Sinsheim. Bao la ushindi la Sweden lilipachikwa katika dakika ya 82 na mchezaji wa kiungo Marie Hammarstrom, aliyeingia uwanjani akiwa mchezaji wa akiba.

Kutokana na kufikia hatua ya nusu fainali, Sweden na Ufaransa zimefanikiwa kujaza nafasi mbili za Ulaya katika michezo ya Olimpik 2012 mjini London, Uingereza. Mbali na rais wa Shirikisho la kandanda la kimataifa FIFA, Sepp Blatter na viongozi wa Shirikisho la kandanda la Ujerumani, Rais wa Ujerumani Christian Wulff pia anatarajiwa kuweko uwanjani kujionea fainali hiyo. Ama kwa mashabiki wa soka, swali ni je, nani atatawazwa bingwa? Marekani itafanikiwa kulinyakua kombe hilo mara ya tatu au ni Japan itakayotawazwa bingwa wa dunia kwa mara ya kwanza? Bila shaka firimbi ya mwisho ndiyo muamuzi.

Mwandishi: Mohammed Abdul-Rahman/AFP,

Mhariri : Prema Martin