1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

EURO 2008 yaingia Nusu Fainali

Kalyango Siraj23 Juni 2008

Italy yatolewa Uhispania yasonga mbele

https://p.dw.com/p/EOhc
Iker Casillas, kulia, akiokoa penalti ya Italy iliopigwa na Daniele De Rossi, kushoto.Picha: AP

Mashindano ya kuwania ubingwa wa soka wa kombe la Ulaya ya mwaka huu yanazidi kupamba moto ambapo robo fainbali imekamilishwa jana kwa vigogo kuangushwa.

Bingwa wa kombe la dunia,Italy ndio imekuwa timu nyingine mashuhuri kutimuliwa kutoka katika mashindano ya kombe la mataifa ya Ulaya yanayoendelea nchini Uswisi na Austria.

Katika mechi ya mwisho ya robo fainali ya kufuzu kwa nusu fainali kwa mashindano hayo Italy ilitolewa na Uhispania kupitia mikwaju ya penalti baada ya mchezo wa kawaida kumalizika kwa sare ya kutofungana bao.

Italy iliboronga penalti mbili na Uhispania ikafaulu kupachika zake 4 na 2 za Italy. Iker Casillas ambae alipangua penalti mbili anasema timu yake ina bahati kushinda mikwaju ya penalti dhidi ya Italy na kuongeza kuwa walichotaka wamekipata.

Hivyo mabingwa wa kombe la dunia Italy wakaaga mashindano hayo kwa shingo upande.

Bila shaka WaHispania iliwabidi watoke uwanjani kichwa juu kutokana na sababu mbili. Kwanza walifuzu kwa nusu fainali na pili jambo ambalo walikuwa hawajalifanya kwa kipindi cha miaka 24.

Pia ushindi dhidi ya Italy ndio wa kwanza katika mashindano makubwa kama hayo nje ya mashindano ya Olimpiki.Pia itakumbukwa kuwa hii ndio mara ya kwanza kwa Uhispania kushinda Italy tangu michezo ya Olimpiki ya mwaka 1920.

Sasa Uhispania itakutana na Urusi katika nusu fainali inayozijumulisha timu nne Urusi ikiwa mojawapo.

Uhispania iliikung'uta Urusi mabao 4 kwa 1 katika mechi ya ufunguzi.Lakini sasa timu ya Urusi ambayo wachezaji wake wengi ni vijana wamejizoazoa na ni wakali.

Urusi ilifuzu baada ya kuilaza Uholanzi katika mechi iliokuwa kali.

Timu nyingine iliofuzu ni Uturuki ambayo inakutana na Ujerumani katika mechi ya ufunguzi wa awamu ya nusu fainali.

Mechi hiyo ni ya Jumatano na ya pili kati ya Urusi dhidi ya Uhispania ni alhamisi.