1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

EU yaiwekea vikwazo Iran.

Halima Nyanza26 Julai 2010

Mawaziri wa mambo ya Nchi za Nje wa Umoja wa Ulaya leo wameidhinisha vikwazo vikali zaidi ya vile vilivyopitishwa na Umoja wa Mataifa hivi karibuni juu ya mpango wa nyuklia wa Iran ulio na utata.

https://p.dw.com/p/OVBf
Rais wa Iran Mahmud Ahmadinejad.Picha: AP

Wamechukua hatua hiyo kwenye mkutano wao uliofanyika mjini Brussels, Ubelgiji.

Mawaziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Umoja wa Ulaya wamepitisha orodha ya vikwazo, baada ya majadiliano mafupi, huku taarifa kuhusiana na vikwazo hivvo vikitarajia kuchapishwa kesho, siku ambayo hatua rasmi zitaanza kuchukuliwa.

Lakini wanadiplomasia tayari wamesema kuwa vikwazo hivyo vitalenga katika mabenki ya Iran, makampuni ya meli na ya ndege pamoja na kupiga marufuku ya kupeleka vifaa na teknolojia kutoka barani Ulaya katika sekta ya mafuta na gesi ya Iran, nchi ambayo  ni ya tano duniani kusafirisha mafuta ghafi, lakini ina uwezo mdogo wa usafishaji.

Mawaziri hao wamesisitiza kuwa madhumuni ya vikwazo hivyo ni kuihammasisha Iran ikubali majadilianio na kukiri kuwa hatua peke yake hazitoshi kuusimamisha mpango huo wa kurutubisha madini ya Uranium.

Hata hivyo mawaziri hao wameonya kuwa  vikwazo hivyo vilivyoweklwa na umoja wa Ulaya vilivyovikali zaidi ya vile vya Umoja wa Mataifa, kwa uopande mwingine vinaweza pia kuathiri makampuni ya Ulaya.

Vikwazo vingi kati ya hivyo, kama vile kuzuia mali za viongozi walio madarakani nchini humo na biashara vitaanza kufanya kazi mara tu vitakapochapishwa katika majarida rasmi ya Umoja wa Ulaya.

Hata hivyo hatua dhidi ya vikwazo vingine vitasubiri kuidhinishwa na mabunge ya nchi, hatua ambayo inaweza kuchukua wiki kadhaa.  

Vikwazo hivyo vinalenga kuishinikiza zaidi Iran kuachana na mradi wake huo wenye utata wa urutubishaji wa madini ya Uranium, mradi ambayo Iran yenyewe inasema kwamba  ni kwa ajili ya matumizi ya amani na kwamba inayohaki ya kuwa na bila ya masharti yoyote, Lakini Umoja wa mataifa unataka Iran isimamishe mradi huo mpaka nchi hiyo itakapothibitisha kwamba haitengenezi silaha za nyuklia.

Akizungumza na Waandishi wa Habari mjini Brussels, kabla ya kupitishwa kwa uamuzi huo, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Uingereza William Hague amesema vikwazo hivyo vinalenga kuishinikiza zaidi Iran kuingia katika majadiliano kuhusiana na mpango wake huo wa nyuklia.

Nao wachambuzi wa mambo wanasema wakati nchi rafiki za Iran kama vile China, Uturuki na Malaysia zinaweza kuchukua hatua za kuipatia nchi hiyo bidhaa, ambazo haitaweza kupata katika nchi za Ulaya, vikwazo vilivyowekwa na nchi za Ulaya bado vina nguvu.

Katika hatua nyingine, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje Ramin Mehmanparast ameushutumu uamuzi huo wa Umoja wa Ulaya kupitisha vikwazo vipya dhidi ya nchi yake, ambavyo vinalenga pia katika sekta ya nishati.

Mwandishi: Halima Nyanza(Reuters, dpa)

Mhariri: Josephat Charo