1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

DW yajibu malalamiko ya msemaji wa Rais Nkurunziza

Mohammed Abdul-Rahman20 Mei 2016

Deutsche Welle yatoa majibu na msimamo kuhusu makala ya Idhaa ya Kifaransa juu ya kusajiliwa kwa wanachama wa tawi la vijana wa chama tawala cha Burundi, "Imbonerakure", iliyomkera afisa mwenye ushawishi serikalini.

https://p.dw.com/p/1IrJQ
Msemaji wa Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi, Bwana Willy Nyamitwe.
Msemaji wa Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi, Bwana Willy Nyamitwe.Picha: DW/J-C Abalo

Mgogoro wa Burundi utajadiliwa wiki hii katika mazungumzo yatakayozishirikisha pande husika katika mji wa kaskazini mwa Tanzania wa Arusha. Jumatatu iliyopita, Umoja wa Mataifa ulitahadharisha juu ya kuongezeka kwa machafuko nchini humo na hali kuzidi kuwa tete.

Hayo na matukio mengine yamekuwa wakati wote yakiripotiwa kwa mapana na Deutsche Welle, lakini baadhi hayawapendezi viongozi wa serikali. Mfano makala ya Idhaa ya Kifaransa ya DW juu ya usajili katika jeshi kwa wafuasi wa Umoja wa Vijana wa chama tawala CNDD-FDD, wanaojulikana kama "Inbonerakure" ambayo imemkasirisha mmoja wa watu mashuhuri serikalini, msemaji wa Rais Pierre Nkurunziza, Bwana Willy Nyamitwe.

Taarifa kama hii ni nyeti kwa Imbonerakure

Yote yalianzia mwishoni mwa juma wakati Idhaa hiyo ilipoamuwa kuripoti kuhusu matukio hayo nchini Burundi. Imbonerakure ambayo maana yake kwa lugha ya Kirundi ni "Wenye kuona mbali" wanashukiwa kuwa ni wanamgambo wanaoutumikia utawala na shutuma hizo za kusajiliwa katika jeshi la polisi na ulinzi zimekuwepo hata kabla ya muanza mgogoro wa kisiasa Aprili 2015, kufuatia tangazo la Rais Nkurunziza kuwa atagombea muhula wa tatu.

Udhibitisho na vyanzo vya taarifa hizi

Taarifa hizi zinatazamwa na maafisa wa serikali kuwa ni nyeti. Kutokana na malalamiko yao, tumeamua kuwafahamisha wasikilizaji wetu juu ya maadili na muongozo wa uhariri wa habari wa Deutsche Welle: muongozo wetu ni kuzihakiki taarifa , vyoanzo vyake na kupata maelezo ya pande zote husika . Ni kutokana na mambo yote hayo ndipo habari fulani inapopewa zingatio. Kuhusiana na kisa hicho cha Ibonerakure na kusajiliwa kwao katika vyombo vya ulinzi vya dola, polisi mmoja ambaye sasa anaishi uhamisho, alikuwa mmojawapo ya vyanzo vilivyodhibitishazoezi hilo. Alisema kundi hilo limekuwa hata na ushawishi mkubwa kuliko maafisa wenye ujuzi wa vyombo vya uasalama vya dola.

Sehemu ya vijana wakati wa machafuko nchini Burundi.
Sehemu ya vijana wakati wa machafuko nchini Burundi.Picha: Getty Images/AFP/A. Vincento

Tangu mapema mwezi Mei, Tume ya Wataalamu ya Umoja wa Mataifa inachunguza machafuko na mauaji nchini Burundi.

Kuwasiliana na maafisa wa serikali ili kupata maelezo yao kuhusu kilichotokea

Hatua ya pili ya kushughulikia uhakiki wa taarifa ni kuwasiliana na maafisa wa serikali kupata maelezo yao. Jum apili ya Mei 15 mwenzetu Eric Topona alimpigia simu Willy Nyamitwe. Mara nyingi mshauri huyo wa mawasiliano na msemaji wa Rais Pierre Nkurunziza amekuwa akitukubali mahojiano. Lakini safari hii alikwenda umbali wa kutukatia simu. Bw Nyamitwe hakusita pamoja na hayo kuelezea kutofurahishwa kwake na baadhi ya ripoti za Idhaa yetu ya Kifaransa. Alisisitiza kwamba "hizo ni habari zinazozingatia uvumi". Mbali na kukata simu, Bw Nyamitwe hakutaka kujibu maswali yetu. Pamoja na hayo kajibu kile tulichokitangaza lakini kwa kupitia mtandao wake wa Twitter.

Nyamitwe ajibu kupitia Twitter

Mara tu baada ya ripoti kurushwa Mshauri huyo wa mawasiliano wa rais Nkurunziza, akatumia mtandao kumshambulia vikali Eric Topona na kusisitiza tena kwamba kilichotangazwa na Idhaa hiyo ya DW kilikuwa si kingine bali "uvumi" tu.

Maandamano dhidi ya Rais Pierre Nkurunziza.
Maandamano dhidi ya Rais Pierre Nkurunziza.Picha: Heinrich-Böll-Stiftung/Igor Rugwiza

Katika hali hii, viongozi wa Deutsche welle wameamua kujibu. Kwanza la msingi ni kuyapinga vikali maelezo ya afisa huyo wa wa Ikulu ya rais wa Burundi. Pia unependa kusisitiza kwamba kampeni ya kuwachafulia jina waandishi habari haibadili ari ya Eric Topona pamoja na wenzetu wengine kote duniani katika kuarifu kinachotokea.

Maadili ya Deutsche Welle

Deutsche Welle inafanya kazi zake za uandishi habari, kwa ari , ujasiri na uhakiki bila ya upendeleo. Inapinda vikali madai ya kwamba inayoripoti kuhusu Burundi yanatokana na uvumi. Inaripoti ukweli wa yanayotokea Burundi. Kampeni ya vitisho dhidi ya waandishi habari haibadili hata kidogo ukweli wa mambo wala kumvunja moyo si Eric Topana wale wenzake wengine kote duniani, katika kusimamia misingi ya uandishi habari. Mashambulizi dhidi ya waandishi habari ni ushahidi wa ulipizaji kisasi kutokana na kuwajibika kwao katika utoaji wa habari huru na zisizoelemea upande wowote - habari zenye ukweli kuhusu kinachoendelea nchini Burundi.

Mojawapo ya hoja za Bw Nyamitwe kwenye mtandao wake wa Twitter ilisema:

Willy Nyamitwe @willynyamitwe

Inconcevable que Eric Topona de @dw_francais ne traite que des faussetés sans fondement et appelle pour nous faire perdre du temps. #Burundi

16:00 - 15 Mai 2016 · Burundi, Burundi

Mwandishi: Mohammed Abdul-Rahman/DW French
Mhariri: Mohammed Khelef