1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

DILI: Upigaji kura waanza nchini Timor Mashariki

9 Aprili 2007
https://p.dw.com/p/CCBF

Raia nusu milioni wa Timor Mashariki wameanza kupiga kura hii leo katika uchaguzi wa rais ambao huenda ukakirejesha madarakani au kukiangusha chama cha mrengo wa kushoto cha Fretilin.

Katika uchaguzi wa kwanza nchini humo tangu uhuru kutoka kwa Indonesia mnamo mwaka wa 2002, maafisa wa uchaguzi watakuwa na kibarua cha kusimamia zoezi la upigaji kura katika vituo 700.

Mgombea wa chama cha Fretilin, Francisco Lu ´Olo Guterres, na mgombea huru Jose Ramos Horta, wanaongoza orodha ya wagombea wanane wanaopigania wadhifa wa urais nchini Timor Mashariki.

Guterres amesema ana hakika chama chake kitashinda baada ya kupiga kura katika kitongoji cha Farol karibu na mji mkuu Dili.

Ushindi wa Guterres huenda ukamuwezesha waziri mkuu wa zamani, Mari Alkatiri, kurejea madarakani wakati wa uchaguzi mkuu utakaofanyika mwezi Juni mwaka huu.

Ikiwa mshindi wa tuzo la amani la Nobel, Ramos Horta atashinda, rais wa sasa, Xanana Gusmao, huenda akawa na nafasi nzuri ya kumshinda Alkatiri katika wadhifa wa waziri mkuu.

Ikiwa hakuna mgombea atakayepata zaidi ya asilimi 50 ya kura, awamu ya pili ya uchaguzi itafanyika tarehe 8 mwezi ujao.