1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Challenge cup-Zanzibar heroes pia nje

Ramadhan Ali19 Desemba 2007

Katika kombe la CECAFA kanda ya Afrika mashariki na kati,Ruanda jana ilizima vishindo vya Zanzibar Heroes.

https://p.dw.com/p/CdjW
Franck Ribery stadi wa B.MunichPicha: AP

Kombe la Ulaya la UEFA linarudi uwanjani jioni hii kwa viongozi wa Ligi wa Ujerumani-Bayern Munich wakikaribisha nyumbani wagiriki Ari Saloniki.Munich yahitaji alao pointi 1 kucheza duru ijayo.Braga ya Ureno ina miadi katika kundi hili F leo na Red Star Belgrade ambayo haina matumaini .

Ama katika kundi E,FC Zurich ya Uswisi inatembelewa nyumbani na Bayer Leverkusen ya Ujerumani.

Katika robo-finali za Challenge Cup- kombe la Afrika Mashariki na kati mjini Dar-es-salaam, Zanzibar Heroes ilipigana jana kufa-kupona na Ruanda,lakini mwishoe ,haikuepuka hatima walioandikiwa na mahasimu wao kutoka Kigali.Kaburi lile lile waliochimbiwa wezao wa Tanzania-bara huko mzizima,walipopapurana na Sudan,ndilo walilozikiwa jana Zanzibar Heroes na kupewa mkono wa buriani.

Tukianza na kombe la CECAFA, Zanzibar Heroes ilikata jana roho kishujaa na kama walivyoanza huko Arusha kishujaa ,walipoondoka sare na mabingwa Sudan 2:2,waliaga mashindano jana pia kishujaa kupitia m ikwaju ya penalty.

George Njogopa anasimulia mambo yalivyokuwa mjini Dar-es-salaam:

Kinyan’ganyiro cha kombe la Afrika la mataifa kikipiga hodi nchini Ghana,Januari 20 ya mwezi ujao,Tunisia imemteua Farid Ben Khalfallah kujiunga na kikosi chao cha kwanza kwa safari ya ghana.Kocha mfaransa Roger Lemerre ametangaza kikosi cha wachezaji 27 hii leo kikijumuisha Ben Khallafah mzaliwa wa Ufaransa.

Tunisia iliotwaa kombe la Afrika la mataifa 2004 iko kundi D pamoja na Angola,Senegal na bafana Bafana –Afrika Kusini.

Kocha wa majirani zao Morocco ,mfaransa mwengine Henri Michel,alichagua jana kikosi cha wachezaji 30 kwa maandalio ya kukabili changamoto ya mwezi ujao huko Accra.Morroco inafungua itajipima kwanza nguvu na Chipolopolo-Zambia hapo Januari 12 kabla ya kucheza na Angola Januari 16. Baada ya hapo ndipo itafunga safari ya accra,Ghana.

Viongozi wa Premier League-ligi ya Uingereza-Arsenal na mahasimu wao wa London ya kaskazini Tottenham hotspurs wameingia nusu-finali ya Kombe la ligi la Uingereza baada ya ushindi wa jana.Arsenal iliikomea Blackburn Rovers 3-2 baada ya kurefushwa mchezo.Tottenham iliichapa manchester city 2-0.

Leo uwanjani katika kombe hili ,Chelsea inavaana na Liverpool.

Na mwishoni kabisa ni habari za kuhuzunisha:Stadi chipukizi wa bundesliga-Ligi ya Ujerumani Abdelazziz Ahnfouf amepatwa na ajali ya motokaa na ameumia vibaya. Motokaa aliokua akiendesha mmorocco huyu mwenye umri wa miaka 27 ilijigonga na kuingia ndani ya lori moja lililokua likitokea Uholanzi.Ahanfouf anaichezea Bielefeld katika Bundesliga na hakufuiatana na timu yake kwa safari ya China.yuko hospitalini akitibiwa.