Brahimi ahimiza mabadiliko ya "kweli" Syria
28 Desemba 2012Lakhdar Brahimi pia anasafiri kuelekea Moscow, Urusi kesho Jumamosi kwa mazungumzo zaidi kuhusu matokeo ya mazungumzo yake na rais wa Syria Bashar al-Assad na wapinzani wake.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Damascus jana baada ya kukamilisha ziara yake ya siku tano nchini Syria, Lakhdar Brahimi alitoa wito wa kuwepo mabadiliko ya kweli ili kumaliza umwagikaji damu unaoendelea nchini humo.
Mkutano wa "B" tatu
Naibu waziri wa Mambo ya kigeni wa Urusi Mikhail Bogdanov amesema watamsikiliza Brahimi na kisha baada ya hapo, huenda kukawa na uamuzi wa kuandaa mkutano mpya wa B tatu, yaani akifanya utani kuhusu herufi ya kwanza ya majina ya mwisho ya wajumbe watakaokutana
Bodganov mwenyewe, Naibu Waziri wa mambo ya nchi za kigeni wa Marekani William Burns na Lakhdar Brahimi wawakilishi wa pamoja wa Umoja wa Mataifa na Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, wamekubaliana kwamba suluhiho la kisiasa kwa mzozo wa Syria ni muhimu na uwezekano wa kufanyika mazungumzo mapema mwezi huu.
Bogdanov amesema mkutano mwingine wa wajumbe hao watatu utafanyika mwezi Januari baada ya likizo. Brahimi ambaye ametoa wito wa kuwepo serikali ya mpito yenye mamlaka nchini Syria kabla ya kufanyika uchaguzi, anajaribu kusimamia mpango wa amani wa kubadilisha madaraka nchini humo, ambako zaidi ya watu 45,000 wameuawa katika uasi dhidi ya miongo minne ya utawala wa familia ya al-Assad.
Madola yamegawanyika kuhusu jukumu la Assad
Jukumu ambalo al-Assad na maafisa wa serikali yake huenda wakapewa matika serikali ya mpito, mpango ambao ulitangazwa katika muafaka wa kimataifa mjini Geneva miezi sita iliyopita, limezigawanya nchi zenye nguvu ulimwenguni.
Juhudi za amani zimesambaratika wakati kile kilichoanza kama maandamano ya amani mwezi Machi mwaka wa 2011 kikigeuka kuwa vita vya wenyewe kwa wenyewe na mapambano ya kimadhehebu kati ya waasi wa Kiislamu wa madhehebu ya Sunni na vikosi vya Assad, vinavyotoka hasa katika madhehebu ya Kishia ya Wa-alawi walio wachache.
Mataifa yenye nguvu ulimwenguni yanaamini kuwa Urusi, ambayo imempa al-Assad msaada wa kijeshi na kidiplomasia kumsaidia dhidi ya uasi unaoendelea, inao ushawishi juu ya serikali ya Syria na ni lazima iwe mchangiaji mkubwa katika mazungumzo ya amani. Moscow imejaribu kujitenga na al-Assad katika miezi ya karibuni na imesema haimuungi mkono, bali inasisitiza kuwa kuondoka al-Assad kutoka madarakani hakuwezi kuwa masharti ya kabla ya mazungumzo. Alhamisi, Waziri wa mambo ya kigeni wa Urusi Sergei Lavrov ameonya kuwa muda unayoyoma kupatikana suluhisho la amani katika mgogoro huo wakati wa mazungumzo na naibu waziri wa mambo ya kigeni wa Syria Faisal Makdad mjini Moscow.
Mwandishi: Bruce Amani/Reuters
Mhariri: Daniel Gakuba