1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Beirut. Viongozi wataka majadiliano.

8 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CClP

Viongozi hasimu wa Lebanon leo wametoa wito wa kurejea katika mazungumzo , wakati upinzani unaoongozwa na chama cha Hizboullah umeapa kutorudi nyuma katika maandamano yake ya mitaani yenye lengo la kuiangusha serikali inayoungwa mkono na mataifa ya magharibi.

Miito hiyo imekuja wakati hali ya wasi wasi inazidi kupanda katika nchi hiyo iliyogawika, wakati upande wa upinzani , ukiongozwa na kundi linaloungwa mkono na Syria na Iran la Hizboullah, likitaka kuendeleza hatua hiyo kwa maandamano.

Upande wa upinzani ambao pia unajumuisha makundi ya Wakristo , umekuwa ukifanya maandamano nje ya ofisi ya waziri mkuu Fouad Siniora katikati ya Beirut, ambako yeye pamoja na mawaziri kadha yamejifungia.

Leo Ijumaa , maelfu ya waumini wa Kishia na Kisunni wamejiunga pamoja katikati ya mji kwa sala katika ishara ya umoja dhidi ya serikali ya Siniora.