1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern, Dortmund wajiandaa kwa "Der Klassiker"

29 Februari 2016

Timu inayoongoza ligi ya Ujerumani – Bundesliga Bayern Munich itaialika Mainz Jumatano wakati nambari mbili Borussia Dortmund ikisafiri kupambana ugenini na Darmstadt

https://p.dw.com/p/1I4MD
Robert Lewandowski gegen Mats Hummels
Picha: Imago

Kisha baadaye fahali hao wawili kukutana katika mpambano mkali maarufu kama DER Klassiker Jumamosi ijayo.

Bayern ina matumaini makubwa baada ya kupata ushindi mgumu wa 2-0 mwishoni mwa wiki dhidi ya Wolfsburg na kuanzisha kile ambacho kocha Pep Guardiola anakitaja kuwa ni “mojawapo ya wiki muhimu za msimu huu”. Bayern hivyo ilijiimarisha kileleni mwa ligi na pengo la point inane mbele ya Dortmund lakini kabla ya kukutana, lazima ipambane na Mainz. Huyu hapa Robert Lewandowski ambaye alifunga goli moja kwenye mechi hiyo likiwa ni lake la 23 msimu huu katika Bundesliga. "Leo ulikuwa mchezo ambao tulistahili kuwa na subira na kucheza kwa kuudhibiti mpira na kujaribu kufunga goli la kwanza. Tulicheza vyema na tumefunga mabao mawili zaidi na kunyakua pointi tatu".

VfL Wolfsburg v FC Bayern Muenchen- Bundesliga
Lewandowski alifunga goli lake la 23 katika BundesligaPicha: Reuters/F. Bimmer

Mainz haistahili kupuuzwa kwa sababu sasa iko katika nafasi ya tano, baada ya kuiduwaza Bayer Leverkusen mabao matatu kwa moja hapo jana.

Dortmund ilitokwa jasho na kupata ushindi wa tatu moja dhidi ya Hoffenheim jana mchuano ambapo kocha wa Hoffenheim alisema walistahili kushinda. "Nadhani katika kipindi cha kwanza tuliutekeleza kikamilifu mpango wetu, tukamsababishia matatizo makubwa mpinzani wetu hasa katika kipindi cha kwanza na tungepaswa kufunga zaidi ya moja bila. Kisha mchezo ukachukua mkondo tafauti. Lakini sasa tutaangazia mchezo dhidi ya Augsburg siku ya Jumatano".

Werder Bremen inayoshikilia nafasi ya 16 ikipambana na Bayer Leverkusen. Pierre-Emerick Aubameyang wa Dortmund pia alifunga goli moja likiwa lake la 22 msimu huu katika Bundesliga. Dormtund sasa inakabiliwa na mchuano mgumu dhidi ya Darmstadt ambao wanapambana kuepuka shoka la kushushwa daraja.

Hapo kesho, nambari tisa atakutana na nambari kumi kwenye ligi, wakati Ingolstadt itaikaribisha Cologne, nao washika mkia Hanover wakipambana na Wolfsburg. Thomas Schaaf alipata ushindi wake wa kwanza akiwa kocha wa Hanover dhidi ya Stuttgart mwishoni mwa wiki. Christian Schulz ni beki wa Hanover. "Ilikuwa muhimu kuwa tumeshinda mchezo leo. Tuliwafikisha kwenye ukuta. Bila shaka leo kulikuwa na bahati nzuri na uhahitaji hilo wakati ukiwa chini. Na sasa hiyo imetuinua na kutupa matumaini kuwa tunaweza kushinda mechi nyingi"

Fußball Bundesliga Borussia Dortmund vs. 1899 Hoffenheim
Aubamayeng alifunga bao lake la 22 katika BundesligaPicha: Getty Images/Bongarts/L. Baron

Hertha Berlin, wanaowashangaza wengi watalenga kujiimarisha katika nafasi ya tatu watakaposhuka dimbani dhidi ya Eintracht Frankfurt huku Borussia Moenchengladbach, wanaoshikilia nafasi ya nne wakiwaalika Stutgart.

Schalke inayosuasua inalenga kuirejesha kwenye mkondo sahihi kampeni yake ya kucheza soka la Ulaya itakapopambana na SV Hamburg, ambao hawajashindwa katika mechi zao nne za mwisho, lakini wameshinda mara moja pekee katika mechi zao tisa za mwisho.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/AP
Mhariri: Mohammed Khelef