1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ASHGABAT : Rais wa Turkmenistan kuzikwa leo

24 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCge

Wananchi wa Turkmenistan leo wanamzika Rais Saparmurat Niyazov ambaye ameitenga nchi hiyo ya Asia ya Kati na ulimwengu na kuitawala kwa mtindo wa ubadhirifu wa kuabudiwa huku tayari kukiwa na dalili za kutokota kwa mapambano ya kuwania kurithi nafasi yake.

Kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 66 amefariki kutokana na mshtuko wa moyo hapo Alhamisi na kuitumbukiza kwenye mashaka nchi hiyo ambayo akiba yake ya gesi ni muhimu kwa Ulaya,Urusi na Marekani.

Mwili wa Niyazov utawekwa kwenye kasri la rais mjini Ashgabat kwa ajili ya ibada ya kumuaga itakayohudhuriwa na maafisa waandamizi wa Turkmenistan na wajumbe wa kigeni.

Maelfu ya Waturkmenistan wanatarajiwa kujipanga barabarani kuangalia msafara utakobeba mwili wa rais huyo kwenda kuzikwa kwenye mji alikozaliwa wa Kipchak.

Turkmenistan iko kwenye siku saba za maombolezo rasmi lakini hakukuweko na huzuni ya wazi ya wananchi kwa mtu ambaye alikandamiza upinzani na kuwatia ndani wanaomkosoa pamoja na kudhibiti kila fani ya maisha ya watu kuanzia mavazi wanayovaa hadi vitabu wanavyosoma.