1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Arsene Wenger kuachia ngazi mwishoni mwa msimu

Sekione Kitojo
20 Aprili 2018

Makocha wa timu za ligi kuu ya England Premier League pamoja na wachezaji wa zamani wamemmiminia sifa kocha wa  Arsenal London Arene Wenger Ijumaa (20.04.2018) baada ya kutangaza atajiuzulu kuifunza timu hiyo.

https://p.dw.com/p/2wPd2
FA-Cup Finale - FC Arsenal - FC Chelsea | Arsene Wenger
Picha: picture-alliance/Offside/M. Atkins

 Wenger  mwenye  umri  wa  miaka 68 alishinda mataji  matatu  ya Premier League  na  vikombe  saba  vya  kombe  la  FA  katika  kipindi  cha miaka  22  akiwa  katika  uongozi  wa  timu  ya  Arsenal lakini  misimu  ya  hivi karibuni  imeamsha hali  ya  kutoridhika miongoni  mwa  mashabiki wakati klabu  hiyo  ilishindwa  kupambana  kuwania  taji  la  ligi.

Arsenal v CSKA Moscow - UEFA Europa League - Quarter Final - Fußball Trainer Wenger
Arsene Wenger kocha wa ArsenalPicha: picture-alliance/empics/A. Davy

Tony Adams , nahodha  wa  Arsenal  wakati  timu  hiyo  iliposhinda  ligi  kuu ya  England Premier League  na  kombe  la  FA  msimu  wa  mwaka  1997 / 98 na  tena  mwaka  2003 / 04   hana  shaka  kuhusiana  na  nafasi  ya kihistoria  ya  kocha  wake  huyo wa zamani katika  klabu  hiyo  ya  mjini London. "Ahsante  kwa  kila  kitu Arsene. Adams  aliandika  katika  ukurasa wa  Instagram.

Kocha  wa  Liverpool Jurgen Klopp amesema  "ameshangaa"  alipokuwa akizungumza  na  waandishi  habari.

"Alikuwa  mtu aliyetamalaki  katikati  ya  miaka  1990 na 2000" Klopp  alisema katika  mkutano  wake  na  waandishi  habari  siku  ya  Ijumaa.  "Ni  tofauti  hivi sasa  kwasababu  tunapaswa  kutoa  changamoto lakini  nchini  Ujerumani alikuwa  mtu  wa  mfano mkubwa," aliongeza  kocha  huyo  raia  wa Ujerumani.

Bildergalerie Sportfoto des Monats März 2018
Arsene Wenger akiiongoza ArsenalPicha: Reuters/D. Klein

Raia  huyo  wa  Ufaransa  anaondoka  katika  uongozi wa  Arsenal  mwaka mmoja  kabla  ya  kumalizika  kwa  mkataba  wake wa  hivi  sasa  wa  miaka miwili. Arsenal  iko  nafasi  ya  sita  katika  Premier League  na  imo  katika nusu  fainali ya  kombe  la  ligi  ya  Ulaya,  Europa League.

Kila la  kheri Wenger

"Baada  ya  kutafakari  kwa  kina  na  kufuatia  majadiliano  na  klabu , nahisi ni  muda  sahihi  wa  kuondoka  mwishoni  mwa  msimu," Wenger  alisema katika  taarifa.

Mmiliki  wa  hisa  kubwa  katika  Arsenal Stan Kroenke  alisema  klabu itamteua  kocha  mpya  haraka  iwezekanavyo.

"Hii  ni  moja  kati  ya  siku  ngumu  sana  katika  miaka  yote  katika  spoti, " alisema  katika  taarifa  ya  klabu  chini  ya  kichwa  cha  maneno "Mercy Arsene"  akiwa  na  maana  ahsante Arsene.

Europa League Arsenal London gegen CSKA Moskau | Jubel
Wachezaji wa Arsenal wakishangiria baoPicha: imago/PA Images/J. Walton

Wenger  aliteuliwa  Oktoba 1, 1996 na  kwa  sasa  ni kocha  aliyetumikia  kwa muda  mrefu  zaidi  katika  Premier League.

"Chochote  kitakachokuja  hapo  baadaye  kwake, hastahili  pungufu  ya shukrani  zetu za  dhati  na  kumtakia  kila  la  kheri kwa  maisha  yake  ya furaha."

Katika  mwaka  2003-04 , Wenger  alikuwa  kocha  wa  kwanza  tangu  mwaka 1888-89 kuiongoza timu  katika  msimu  mzima  wa  ligi  ya juu  bila kufungwa.

"Katika  mwaka  huo  tulikuwa  tunajaribu  tu kuwa  mabingwa," Thierry Henry , mfungaji  mashuhuri  wa  klabu  hiyo  aliiambia televisheni  ya   michezo  ya Sky.

Fußball Skyexperte Thierry Henry
Mchezaji wa muda mrefu wa Arsenal Thierry HenryPicha: Getty Images/M. Regan

"Alikuwa  anatuambia  wakati  tayari  ni  mabingwa, "vijana  mnaweza  kufanya kitu  cha  kushangaza."

Wenger  alishinda  taji  lake  la  saba  la  kombe  la  FA msimu  uliopita, wakati  Arsenal  ikiishinda  Chelsea  kwa mabao  2-1  uwanjani Wembley, lakini  kikosi  chake  kilishindwa  kufikia  kucheza katika  Champions League kwa  mara  ya  kwanza  katika  muda  wa  miaka  17, na  kumekuwa  na  hali ya  kutoridhika  miongoni  mwa  sehemu  ya  mashabiki  wa  Arsenal, ambao wamekuwa  wakitoa  miito  ya  Wenger  kuondoka.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / dpae