1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Amnesty Int: Mkuu wa jeshi la Myanmar ana kesi ya kujibu ICC

Sylvia Mwehozi
27 Juni 2018

Shirika la Amnesty International limetaka mkuu wa jeshi la Myanmar na maafisa wengine 12 wa ngazi ya juu, kufikishwa katika mahakama ya kimataifa ya uhalifu kwa madai ya kutenda uhalifu dhidi ya binadamu. 

https://p.dw.com/p/30Mcl
Myanmar Armee Chef Min Aung Hlaing
Picha: picture-alliance/dpa/V. Savitsky

Myanmar imekabiliwa na ukosoaji wa kimataifa na madai ya safisha safisha ya kikabila baada ya Warohingya 700,000 katika jimbo la Rakhine kukimbilia katika nchi jirani ya Bangladesh tangu mwezi Agosti.

Madai yalioenea ya ubakaji, uchomaji moto na mauaji ya kiholela yaliyofanywa na vikosi vya kijeshi na waumini wa madhehebu ya Budha katika jimbo la Rakhine, yamekanushwa kwa kiasi kikubwa na pande zote za kiraia na kijeshi za serikali ya Myanmar.

Jeshi la Myanmar linashutumiwa kutenda makosa 9 kati ya 11 dhidi ya binadamu yaliyo orodheshwa katika mkataba wa Roma wa mahakama ya ICC, kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na shirika la Amnesty International.

Ushahidi uliokusanywa

Bangladesch Rohingya auf der Flucht aus Myanmar
Kambi ya wakimbizi wa Warohingya mpakani na BangladeshPicha: Getty Images/AFP/M. Uz Zaman

Shirika hilo lenye makao makuu yake jijini London, limelitolea mwito Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa, kuwafikisha wahusika katika mahakama ya ICC kwa uchunguzi, likibainisha ushahidi ilioukusanya katika uchunguzi wa miezi tisa. Mkurugenzi wa kukabiliana na migogoro kutoka shirika hilo Tirana Hassan anasema, "vurugu zilizofanywa wakati wa operesheni za safisha safisha mwaka 2017 hazijawahi kutokea kwa kiwango na ukatili wake. Na bila shaka huu ni uhalifu dhidi ya ubinadamu.Tunazungumzia juu ya ubakaji, mauaji, mateso, njaa, matumizi ya mabomu, kiwango kikubwa cha uchomaji moto vijiji.Huu ni uhalifu ambao ni mbaya kiasi kwamba wanapaswa kufikishwa mahakama ya uhalifu."

Amnesty International linaamini kwamba kulingana na ushahidi, kwamba ukandamizaji huo ulikuwa umepangwa na kuratibiwa dhidi ya Warohinya. Mshauri mwandamizi Matthew Wells ameongeza kuwa, "hatimaye, kwa pamoja, ushahidi huu umeturuhus kutaja watu 13 maalum ambao tuna ushahidi wa kuonyesha kwamba wanapaswa kukabiliwa na mashitaka ya uhalifu dhidi ya ubinadamu. Na hii ni kutoka kwa watu ambao walifanya mateso, ambao walihusika katika mauaji, kwa makamanda ambao walisimamia vitengo hivyo na hatimaye kwa mkuu wa jeshi mwenyewe, Jenerali Min Aung Hlaing ambaye tunaamini anapaswa kujibu kwa amri yake ya uhalifu dhidi ya binadamu"

Matthew Wells
Mathew Wells kutoka Amnesty International Picha: Amnesty International

Shinikizo kutoka Jumuiya ya kimataifa

Jumuiya ya kimataifa imeanza kuiandamana Myanmar lakini maafisa wake wanakana madai kwamba jeshi lilitenda uhalifu. Umoja wa Ulaya siku ya Jumatatu ulitangaza kuwawekea vikwazo maafisa saba kuhusiana na ukiukaji wa haki za binadamu dhidi ya Rohingya. Majaji katika mahakama ya ICC tayari wameieleza Myanmar kujibu ombi la mashitaka ili kuzingatia usikilizaji wa kesi kwa madai ya kuwakimbiza Warohingya kwenda nchi jirani ya Bangladesh ifikapo Julai 27.

Msemaji wa serikali Zaw Htay alivieleza vyombo vya habari vya ndani wiki kwamba Myanmar ambayo si mwanachama wa ICC  haina sababu ya kutoa majibu. Lakini baraza la usalama la Umoja wa Mataifa lilisema kwamba ICC inaweza kuanzisha kesi ya kisheria dhidi ya maafisa wa kijeshi hata kama Myanmar sio mwanachama.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/dpa

Mhariri: Iddi Ssessanga